Hamia kwenye habari

AGOSTI 9, 2016
ARMENIA

Mashahidi wa Yehova wa Kwanza Kuandikishwa Kwenye Programu ya Utumishi wa Badala wa Kiraia Nchini Armenia Wamaliza Wajibu Wao

Mashahidi wa Yehova wa Kwanza Kuandikishwa Kwenye Programu ya Utumishi wa Badala wa Kiraia Nchini Armenia Wamaliza Wajibu Wao

Kikundi cha kwanza cha Mashahidi vijana nchini Armenia kilichonufaika na mpango wa utumishi wa badala wa kiraia wamejitahidi kufanya kazi kwa bidii ili kutimiza wajibu wao kwa taifa. Wakati uliopita vijana wengi walifungwa gerezani kwa kukataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Hata hivyo, mwaka wa 2013 Jamhuri ya Armenia ilifanya marekebisho ya sheria yake ili vijana hao wafanye utumishi wa kiraia badala ya utumishi wa kijeshi. Kufikia sasa, zaidi ya Mashahidi 200 wameandikishwa kwenye mpango huo. Mashahidi 16 tayari wamemaliza utumishi wao kwa taifa kufikia mwishoni mwa mwezi Juni 2016.

Mafanikio ya Utumishi wa Badala wa Kiraia

Mashahidi vijana ambao wamemaliza utumishi wao wa kiraia katika programu hii, mwanzoni walifungwa gerezani kwa sababu ya kukataa kujiandikisha jeshini. Sheria mpya ilipoanza kutumiwa, walitolewa gerezani na kuandikishwa kwenye mpango huo wa utumishi wa badala wa kiraia. Kufikia Januari 2014, walianza kufanya kazi kama vile kutengeneza bustani, kusafisha barabara, kuwasaidia wahudumu wa afya kwenye vituo vya afya, au kutoa huduma nyingine.

Vijana waliomaliza utumishi wao wa badala wa kiraia wanafurahi kwamba serikali iliwapa nafasi ya kufanya utumishi wenye maana, uliotia ndani kurembesha mazingira na kutoa huduma kwa wenye uhitaji. Kupitia mpango huu mpya, vijana waliomaliza wajibu wao wataendelea kuwa washiriki wazuri wa jamii bila shutuma ya kuwa na rekodi ya uhalifu.

Davit Arakelyan, mwenye umri wa miaka 22, ambaye amemaliza utumishi wake wa badala wa kiraia aliopangiwa kwenye hospitali ndogo, alisema hivi: “Utumishi wa badala umenisaidia kuwa makini zaidi, kuwajibika, na kufanya kazi kwa bidii. Ninafurahi kutimiza wajibu wangu kwa taifa kwa njia ambayo kwa kweli iliwasaidia wengine. Viongozi na wafanyakazi kwenye hospitali hiyo ndogo na hata baadhi ya wakazi wa eneo hilo walitupongeza kwa kufanya kazi nzuri.” Mikhayil Manasyan, ambaye pia ana umri wa miaka 22, alipangiwa kazi kwenye Wizara ya Hali za Dharura. Alisema hivi: “Nimejifunza ustadi mpya nilipokuwa nikitoa huduma, na sasa hii inaweza kuwa kazi yangu. Nilitimiza utumishi wangu kwa taifa bila kuiumiza dhamiri yangu.”

Je, Mambo Ambayo Armenia Imejionea Yatazichochea Nchi Nyingine Kukubali Utumishi wa Badala wa Kiraia?

Karibuni, nchi ya Armenia imechukua hatua ya ziada ya kurekebisha katiba yake ili kutambua haki za wale wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Kifungu namba 41(3) cha marekebisho ya katiba, ambacho kilianza kutumiwa Desemba 2015, kilisema hivi: “Kila raia ambaye utumishi wa kijeshi unapingana na dini au imani yake ana haki ya kufanya utumishi wa badala wa kiraia kwa kufuata utaratibu ulioamriwa katika sheria.” Washauri wa Baraza la Ulaya wameisifu Armenia kwa kuchukua hatua hii, ambayo waliita “njia iliyojitokeza [ambayo] inapaswa kusifiwa ya kutekeleza hukumu ya kesi ya Bayatyan v. Armenia a.

Programu hii ya utumishi wa badala wa kiraia imefanya Armenia itimize viwango vya kimataifa. Armenia imefanya maendeleo kutoka kuadhibu mpaka kuheshimu haki za uhuru wa dhamiri za wale wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Faida ya sera hii ni kwamba inatoa mfano bora kwa nchi zinazowapa adhabu wale wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Mambo ambayo Armenia imejionea yanaonyesha kwamba kutekeleza programu hii kunaweza kutosheleza mahitaji ya serikali na raia.

Akizungumza kwa niaba ya Mashahidi wa Yehova nchini Armenia, Tigran Harutyunyan alisema hivi: “Tunafurahi kwamba serikali ya Armenia imechukua hatua inayofaa kuhakikisha inatetea haki za msingi za wanadamu, kutia ndani haki ya watu wanaokataa kujiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri. Sasa, Mashahidi vijana nchini Armenia wanaweza kutimiza wajibu wao serikalini kwa njia ambayo inawafanya waheshimu dhamiri zao na kuwanufaisha wengine.”

a Bayatyan v. Armenia ([GC], na. 23459/03, ECHR 2011) uamuzi muhimu uliofanywa kwenye Baraza Kuu la Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu. Kwa mara ya kwanza, Mahakama ilitoa uamuzi ulioonyesha kwamba haki ya kutojiunga na jeshi kwa sababu ya dhamiri inapaswa kutambuliwa kama inavyoelezwa kwenye Kipengele cha 9 (uhuru wa mawazo, dhamiri, na dini) cha Mkataba wa Ulaya wa Haki za Kibinadamu.