Hamia kwenye habari

Biblia Inasema Nini Kuhusu Urafiki?

Biblia Inasema Nini Kuhusu Urafiki?

Jibu la Biblia

 Urafiki unaweza kutufanya tuwe na maisha yenye furaha na mafanikio. Marafiki wazuri huwa na uvutano mzuri kwa wenzao na kuwasaidia kuboresha sifa zao nzuri.—Methali 27:17.

 Hata hivyo, Biblia inakazia umuhimu wa kuchagua marafiki kwa uangalifu. Inaonya kuhusu madhara ya kuwa na marafiki wasiofaa. (Methali 13:20; 1 Wakorintho 15:33) Marafiki kama hao wanaweza kumwongoza mtu afanye maamuzi ya kipumbavu au kuharibu sifa zake nzuri.

Katika makala hii

 Ni nini kinachomfanya mtu kuwa rafiki mzuri?

 Biblia inafundisha kwamba urafiki mzuri haupaswi kutegemea tu mapendezi yanayofanana. Kwa mfano, Zaburi 119:63 inasema: “Mimi ni rafiki ya wote wanaokuogopa wewe a na ya wale wanaoyatii maagizo yako.” Ona kwamba mwandikaji wa Biblia anasema kwamba anachagua marafiki wanaoogopa kumchukiza Mungu na wanaotamani kuishi kupatana na viwango vya Mungu.

 Pia, Biblia inaonyesha sifa ambazo rafiki mzuri anapaswa kuwa nazo. Kwa mfano:

  •   “Rafiki wa kweli hupenda nyakati zote naye ni ndugu ambaye amezaliwa kwa ajili ya nyakati za taabu.”—Methali 17:17.

  •   “Kuna marafiki walio tayari kuangamizana, lakini kuna rafiki anayeshikamana na mtu kwa ukaribu kuliko ndugu.”—Methali 18:24.

 Mistari hii inafundisha kwamba rafiki mzuri ni mshikamanifu, mwenye upendo, fadhili, na ukarimu. Rafiki wa kweli anategemeka, na yuko tayari kutoa msaada kunapokuwa na matatizo. Pia, rafiki wa kweli atakuwa na ujasiri wa kutosha kutuambia tunapoanza kupotea au tunapokaribia kufanya uamuzi usiofaa.—Methali 27:6, 9.

 Kuna mifano gani ya marafiki wazuri katika Biblia?

 Biblia ina mifano ya marafiki wazuri kati ya watu waliotofautiana umri, malezi, utamaduni, na cheo. Fikiria mifano mitatu.

  •   Ruthu na Naomi. Ruthu alikuwa binti-mkwe wa Naomi, na huenda Naomi alikuwa na umri mkubwa sana kuliko Ruthu. Mbali na hilo, Ruthu alilelewa katika utamaduni tofauti na Naomi. Licha ya tofauti hizo, walikuwa na urafiki wa karibu sana na wenye upendo.—Ruthu 1:16.

  •   Daudi na Yonathani. Ingawa Yonathani alimzidi Daudi umri kwa miaka 30, Biblia inasema kwamba Daudi na Yonathani “[walishikamana] na kuwa marafiki wa karibu sana.”—1 Samweli 18:1.

  •   Yesu na mitume wake. Yesu alikuwa na mamlaka juu ya mitume wake, kwa kuwa alikuwa mwalimu na bwana wao. (Yohana 13:13) Hata hivyo, hakuhisi alikuwa bora hivi kwamba hawakustahili kuwa rafiki zake. Badala yake, Yesu alikuwa na uhusiano wa karibu na wale waliofuata mafundisho yake. Alisema hivi: “Nimewaita rafiki, kwa sababu nimewajulisha mambo yote niliyosikia kutoka kwa Baba yangu.”—Yohana 15:14, 15.

 Je, mwanadamu anaweza kuwa rafiki ya Mungu?

 Ndiyo, inawezekana kwa wanadamu kuwa rafiki za Mungu. Biblia inasema hivi: “Ana urafiki wa karibu na watu wanyoofu.” (Methali 3:32) Kwa maneno mengine, Mungu anawachagua watu safi, wanyoofu, wanaoheshimika, na wanaojitahidi kuishi kulingana na viwango vyake vya mema na mabaya. Kwa mfano, Maandiko yanamtaja mwanamume mwaminifu Abrahamu kihususa kuwa rafiki ya Mungu.—2 Mambo ya Nyakati 20:7; Isaya 41:8; Yakobo 2:23.

a Muktadha wa zaburi hii unaonyesha kwamba neno “wewe” katika mstari huu linamrejelea Mungu.