Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MSAADA KWA AJILI YA FAMILIA | VIJANA

Mzazi Anapokufa

Mzazi Anapokufa

CHANGAMOTO

Dami alikuwa na umri wa miaka sita baba yake alipokufa kwa sababu ya kutanuka kwa mshipa wa damu. Derrick alikuwa na miaka tisa alipofiwa na baba yake kutokana na ugonjwa wa moyo. Naye Jeannie alikuwa na miaka saba mama yake alipokufa baada ya kuugua kansa ya kizazi kwa mwaka mmoja. *

Bila kutazamia, vijana hao watatu walifiwa na watu waliowapenda. Je, umewahi kukabili hali kama hiyo? Ikiwa ndivyo, makala hii itakusaidia kuona jinsi unavyoweza kukabiliana na kifo cha mpendwa wako. * Kwanza kabisa, hebu tuchunguze mambo machache kuhusu huzuni ya kufiwa.

MAMBO UNAYOHITAJI KUJUA

Huzuni huonyeshwa kwa njia tofauti-tofauti. Hilo linamaanisha kwamba huenda jinsi unavyohuzunika ni tofauti na wengine. Kitabu Helping Teens Cope With Death kinasema hivi: “Hakuna njia fulani hususa au sheria zilizowekwa za jinsi ya kukabiliana na kifo.” Jambo muhimu ni kutozuia kuonyesha huzuni yako. Kwa nini? Kwa sababu . . .

Ni hatari kuzuia kuonyesha huzuni. Jeannie, aliyetajwa mapema anasema hivi: “Nilifikiri kwamba nilipaswa kuwa imara ili nimfariji mdogo wangu, hivyo nilizuia hisia zangu. Hadi leo, mimi huficha mambo yanayoumiza, ingawa jambo hilo halifai.”

Wataalamu wanakubaliana na hilo. Kitabu The Grieving Teen kinasema hivi: “Hisia haziwezi kufichwa au kuzuiwa milele. Baadaye hisia hizo hujitokeza zikiwa hasira au ugonjwa mwingine hasa wakati usiotazamiwa.” Pia, kuzuia huzuni kunaweza kusababisha matumizi mabaya ya kileo au dawa ili kutuliza uchungu wa moyoni.

Huenda huzuni ikaambatana na hisia zisizoeleweka. Kwa mfano, baadhi ya watu humkasirikia mtu aliyekufa, wakihisi kwamba “amewatelekeza.” Wengine humlaumu Mungu kwa kutozuia kifo cha mpendwa wao. Wengi wanaohuzunika huhisi hatia kwa sababu ya mambo waliyotenda au kusema kwa aliyekufa kwa kuwa hawawezi kuyasuluhisha tena.

Kwa kweli, kuhuzunika ni hali isiyoweza kuelezwa kwa urahisi. Unawezaje kupata faraja na msaada utakaokusaidia kusonga mbele?

MAMBO UNAYOWEZA KUFANYA

Zungumza na mtu mwingine. Huenda ukahisi kwamba ni bora ujitenge na watu katika kipindi hicho kigumu. Hata hivyo, kueleza hisia zako kwa rafiki au mshiriki wa familia kutakusaidia na hivyo kuepuka kulemewa zaidi na hisia hizo.—Kanuni ya Biblia: Methali 18:24.

Andika mawazo yako. Andika mambo unayokumbuka kuhusu mzazi wako aliyekufa. Kwa mfano, ni jambo gani la pekee linalofanya umkumbuke? Andika sifa zake unazozipenda. Ni sifa gani ungependa kuiga maishani mwako?

Unapolemewa na mawazo mabaya, kwa mfano, labda unafikiria mambo yasiyofaa ambayo uliwahi kumwambia mzazi wako kabla hajafa, andika vile unavyohisi na kwa nini unahisi hivyo. Kwa mfano, “Ninahisi hatia kwa sababu tulishindwa kuelewana na baba siku moja kabla ya kifo chake.”

Pili, uwe na usawaziko kuhusu hisia za hatia. Kitabu The Grieving Teen kinaeleza hivi: “Huwezi ukajilaumu kwa kosa ambalo hukujua kwamba hutapata fursa ya kuomba msamaha kulihusu. Ni jambo lisilopatana na akili kuwa na maoni ya kwamba mtu hapaswi kusema au kutenda jambo ambalo litafanya baadaye aombe msamaha.”—Kanuni ya Biblia: Ayubu 10:1.

Tunza afya yako. Pumzika vya kutosha, fanya mazoezi kwa ukawaida na ule vyakula vyenye lishe. Ikiwa huna hamu ya kula, panga kula chakula chepesi mara nyingi, badala ya kula chakula kizito kwa wakati mmoja. Fanya hivyo hadi hamu ya kula itakaporudia hali yake ya kawaida. Usitulize huzuni yako kwa kula vyakula visivyo na lishe au kunywa pombe kwa kuwa hilo litafanya hali iwe mbaya zaidi.

Zungumza na Mungu kupitia sala. Biblia inasema hivi: “Mtupie Yehova mzigo wako, naye mwenyewe atakutegemeza.” (Zaburi 55:22) Sala si njia tu ya kutuliza hisia. Ni mazungumzo halisi na Mungu ambaye “hutufariji katika dhiki yetu yote.”—2 Wakorintho 1:3, 4.

Njia moja ambayo Mungu hutumia kuwafariji wale wanaoomboleza ni kupitia Neno lake, Biblia. Chunguza yale ambayo Biblia inafundisha kuhusu hali ya wafu na tumaini la ufufuo. *Kanuni ya Biblia: Zaburi 94:19.

^ fu. 4 Pia, unaweza kusoma masimulizi ya Dami, Derrick, na Jeannie katika makala inayofuata.

^ fu. 5 Ingawa makala hii inazungumzia kifo cha mzazi, kanuni hizi zinaweza kutumika inapohusu kifo cha mtu yeyote wa familia au rafiki.

^ fu. 19 Soma sura ya 16 ya kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1. Unaweza kukipakua bila malipo kwenye tovuti ya www.mt1130.com/sw. Tafuta kwenye MACHAPISHO.