Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Biblia Inazungumzia Nini?

Biblia Inazungumzia Nini?

Biblia Inazungumzia Nini?

WENGINE huona Biblia kuwa kitabu cha historia, kwa kuwa ina maelfu ya rekodi ya jinsi Mungu alivyoshughulika na wanadamu. Wengine hukiona kuwa kitabu kinachozungumzia kanuni za maadili. Wanataja sheria na kanuni zaidi ya 600 zilizohusu mambo ya kihukumu, kifamilia, kiadili, na ya kidini ambayo Mungu alilipa taifa la Israeli. Na wengine huiona Biblia kuwa kitabu kinachotoa mwongozo wa kiroho na kinachofunua akili ya Mungu.

Kwa kweli, ufafanuzi huo wote ni sahihi. Biblia inasema hivi: “Andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo, kwa kutia nidhamu katika uadilifu, ili mtu wa Mungu awe na uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, 17) Bila shaka, kila kitu katika Neno la Mungu, kutia ndani masimulizi ya kihistoria, sheria, na mashauri ya kiroho, ni chenye thamani.

Hata hivyo, Biblia ni zaidi tu ya mkusanyo wa habari zenye manufaa. Biblia ni ufunuo kutoka kwa Yehova Mungu. Inatoa mashauri yanayofaa, yaliyoongozwa na roho kwa ajili ya maisha ya kila siku. Pia inafunua kusudi la Yehova kwa ajili ya dunia na wanadamu, na vilevile inaonyesha jinsi atakavyoondoa vitu vinavyowafanya wanadamu wateseke. Jambo muhimu zaidi, Biblia inaeleza kwamba ukweli kuhusu Mungu umepotoshwa na inatuambia jinsi atakavyotatua suala hilo la ulimwenguni pote.

Mungu Anaitwa Mwongo na Mtawala Mbaya

Biblia inasema kwamba Mungu aliwaumba wanadamu wa kwanza, Adamu na Hawa, wakiwa na akili na miili mikamilifu na kuwaweka katika mazingira yanayofaa. Aliwaweka wasimamie dunia na wanyama. (Mwanzo 1:28) Wakiwa watoto wa Mungu, Adamu na Hawa walikuwa na nafasi ya kuishi milele duniani iwapo wangemtii Baba yao wa kimbingu. Aliwapa sheria moja tu. Yehova alisema: “Matunda ya kila mti wa bustani unaweza kula mpaka ushibe. Lakini kuhusu matunda ya mti wa ujuzi wa mema na mabaya usile, kwa maana siku utakapokula, utakufa hakika.”—Mwanzo 2:16, 17.

Hata hivyo, kiumbe wa roho anayetajwa katika Biblia kuwa Shetani Ibilisi, alisema kinyume cha hilo: “Hakika hamtakufa.” (Mwanzo 3:1-5) Akimpinga Mungu bila aibu, Shetani alisema kwamba Muumba ni mwongo na kuwa njia Yake ya kutawala ilikuwa mbaya, kwamba mwanadamu angeishi vizuri bila Mungu. Shetani alimsadikisha Hawa kwamba kutomtii Mungu kungempa uhuru na angeweza kujiamulia jinsi atakavyoishi. Alisema kwamba Hawa angekuwa “kama Mungu”! Hivyo, Shetani alishambulia jina zuri la Yehova na kusudi lake.

Mazungumzo hayo yalikuwa na matokeo mabaya sana. Kwa kweli, kusudi la Yehova la kuondoa lawama iliyowekwa juu ya jina na sifa yake, ndicho kichwa kikuu cha Biblia. Hilo linaelezwa katika sala ya mfano ya Yesu ambayo mara nyingi huitwa Sala ya Bwana au Sala ya Baba Yetu. Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasali hivi: “Jina lako na litakaswe, Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani.”—Mathayo 6:9, 10.

Jinsi Mungu Anavyoliondolea Jina Lake Lawama

Shetani alizusha masuala muhimu: Ni nani aliyesema kweli kati yake na Yehova? Je, Yehova anatawala uumbaji wake kwa haki na kwa njia inayofaa? Je, ana haki ya kuwatazamia wanadamu wamtii? Je, wanadamu wangefaidika zaidi kwa kujitawala? Ili kujibu maswali hayo, Yehova amewaruhusu wanadamu wajitawale kwa muda.

Matokeo yamekuwa nini? Tangu uwongo huo wa kwanza uliposemwa huko Edeni, historia ya wanadamu imejawa na hali ngumu na matatizo, ikithibitisha kwamba Shetani ni mwongo mkubwa sana na kwamba kutomtegemea Mungu hutokeza tu msiba. Hata hivyo, Yehova akiwa na upendo na hekima isiyo na mipaka anakusudia kuliondolea jina lake lawama kwa kuondoa shida zote zilizoanzia Edeni. Atafanya hivyo kwa kutumia Ufalme wa Kimasihi. Ufalme huo ni nini?

Mungu Atasuluhisha Mambo Kupitia Ufalme

Mamilioni ya watu hukariri kwa ukawaida Sala ya Bwana. Hebu tumia muda fulani utafakari kuhusu maana ya sala hiyo. Fikiria maneno haya: “Ufalme wako na uje.” (Mathayo 6:10) Ufalme huo si hali tu ya moyoni, kama ambavyo wengine husema. Badala yake, kama neno “-falme” linavyodokeza, hiyo ni serikali ya kimbingu iliyo chini ya Yesu Kristo, “Mfalme wa wafalme.” (Ufunuo 19:13, 16; Danieli 2:44; 7:13, 14) Biblia inafundisha kwamba atatawala juu ya dunia, akifanya kuwe na amani na umoja wa kudumu kati ya watu wote na kuondoa uovu wote duniani. (Isaya 9:6, 7; 2 Wathesalonike 1:6-10) Kwa njia hiyo, Ufalme wa Mungu, na si serikali yoyote ya kibinadamu, utatimiza maneno ya Yesu: “Mapenzi yako na yatendeke duniani.”

Ili kuhakikisha kwamba maneno hayo yanatimizwa, Yesu alitoa uhai wake kuwa fidia ili kuwakomboa wazao wa Adamu kutoka katika dhambi na kifo. (Yohana 3:16; Waroma 6:23) Hivyo, chini ya Ufalme wa Mungu, wote wanaoonyesha imani katika dhabihu ya Kristo watashuhudia madhara ya dhambi ya Adamu yakiondolewa na wanadamu wakifikia ukamilifu hatua kwa hatua. (Zaburi 37:11, 29) Hatimaye udhaifu unaotukabili hasa tunapozeeka, utaondolewa. Hata uchungu wa kihisia unaowapata wanadamu kwa sababu ya ugonjwa na kifo utakuwa ‘umepitilia mbali.’—Ufunuo 21:4.

Tunawezaje kuwa na hakika kwamba Mungu atatimiza ahadi zake? Sababu moja ni kwamba mamia ya unabii katika Biblia tayari yametimizwa. (Ona ukurasa wa 9.) Kwa wazi basi, imani yetu katika Biblia haitegemei mambo ambayo hayajathibitishwa, bali inategemea mambo hakika na uthibitisho mwingi.—Waebrania 11:1.

Mashauri Yanayofaa Siku Zetu

Zaidi ya kutoa msingi thabiti wa kuwa na tumaini hakika kwa ajili ya wakati ujao, pia Biblia inatusaidia kufurahia maisha zaidi leo. Kwa mfano, Neno la Mungu linatoa mashauri yasiyo na kifani kuhusu ndoa, maisha ya familia, mahusiano kati ya wanadamu, kupata furaha, na mambo mengine mengi. Fikiria mifano michache tu.

Fikiria kabla ya kusema. “Kuna mtu anayesema bila kufikiri kama kwa upanga unaochoma, lakini ulimi wa mwenye hekima huponya.”—Methali 12:18.

Epuka wivu. “Moyo mtulivu ni uzima wa mwili wenye nyama, lakini wivu hufanya mifupa iwe na ubovu.”—Methali 14:30.

Watie nidhamu watoto wako. “Mlee mvulana kulingana na njia inayomfaa; hata atakapozeeka hatageuka kando na kuiacha.” “Mvulana aliyeachiliwa atamletea mama yake aibu.”—Methali 22:6; 29:15.

Uwe mwenye kusamehe. Yesu alisema: “Wenye furaha ni wale walio na rehema, kwa kuwa wataonyeshwa rehema.” (Mathayo 5:7) Mfalme Sulemani mwenye hekima aliandika hivi: “Upendo hufunika hata makosa yote.” (Methali 10:12) Ikiwa dhambi ambayo mtu amekufanyia ni kubwa hivi kwamba huwezi tu kumsamehe na kusahau, Biblia inashauri hivi: “Nenda ufunue kosa lake kati yako na yeye peke yake.”—Mathayo 18:15.

Epuka kupenda pesa. “Kupenda pesa ni chanzo cha mambo mabaya ya namna zote, na kwa kujitahidi kufikia upendo huo wengine . . . wamejichoma wenyewe kila mahali kwa maumivu mengi.” (1 Timotheo 6:10) Ona kwamba Biblia inashutumu “kupenda pesa,” lakini haishutumu pesa zenyewe.

“Barua” Kutoka kwa Baba Yetu wa Mbinguni

Hivyo, Biblia inazungumza kuhusu mambo mengi. Kama tulivyoona, inazungumza hasa kuhusu Mungu na kusudi lake. Lakini inazungumza pia kuhusu sisi, wanadamu, na jinsi tunavyoweza kuishi kwa furaha sasa na milele chini ya utawala wa Ufalme wa Mungu. Kwa njia fulani, Biblia ni kama barua kutoka kwa ‘Baba yetu aliye mbinguni,’ Yehova. (Mathayo 6:9) Kupitia Biblia, Yehova ametueleza mawazo yake yenye thamani na kutufunulia mapenzi yake na utu wake wenye kupendeza.

Kwa kusoma Biblia na kutafakari kuihusu, tunaanza “kumwona” Mungu jinsi alivyo hasa. Mioyo yetu huvutiwa kwake katika kifungo chenye upendo cha muungano. (Yakobo 4:8) Kwa hakika, Biblia inazungumzia mengi zaidi kuliko historia, unabii, na sheria. Inazungumzia pia uhusiano wa karibu, naam, uhusiano wetu wa kibinafsi pamoja na Mungu. Jambo hilo linafanya kitabu hicho kuwa cha pekee na chenye thamani sana.—1 Yohana 4:8, 16.

[Blabu katika ukurasa wa 19]

Kichwa kikuu cha Biblia kinaelezwa vizuri sana katika sentensi za kwanza chache za sala ya mfano ya Yesu

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 21]

JINSI YA KUSOMA BIBLIA

Inafurahisha kusoma Biblia. Kwa kweli, masimulizi na masomo yake yanajulikana sana hivi kwamba yanapatikana katika vitabu vya lugha nyingi. Biblia inatusaidia kumfahamu Muumba wetu, Yehova Mungu. Pia ni chanzo cha hekima nyingi yenye manufaa. Methali moja ya Biblia inasema: “Hekima ndilo jambo kuu. Jipatie hekima; na pamoja na vyote unavyojipatia, jipatie uelewaji.” (Methali 4:7) Unaweza kupataje manufaa mengi unaposoma Biblia?

Jaribu kusoma wakati akili yako inapokuwa chonjo zaidi. Na usisome tu haraka-haraka. Lengo lako linapaswa kuwa kujaza akili yako mawazo ya Mungu na kuyachanganua. Baada ya kusoma, tafakari kuhusu yale ambayo umesoma, na uyalinganishe na yale ambayo tayari unafahamu. Kufanya hivyo kutaongeza uelewaji na uthamini wako.—Zaburi 143:5.

Huenda wengine wakajiuliza, ‘Nianze kusoma Biblia kuanzia wapi?’ Bila shaka, unaweza kuanzia mwanzo. Hata hivyo, watu fulani wanaposoma Biblia kwa mara ya kwanza huona ni rahisi kuanza kwa kusoma Injili, vitabu ambavyo vinazungumzia maisha na huduma ya Yesu, yaani, Mathayo, Marko, Luka, na Yohana. Kisha wengine hufuatia kusoma vitabu vya kishairi vilivyoandikwa kwa njia ya kupendeza na vilivyojaa hekima, yaani, Zaburi, Methali, na Mhubiri. Baada ya kufanya hivyo, hamu yako itakuwa imeamshwa ili usome sehemu nyingine za Biblia. (Ona chini.) Na usiwe na wazo lililopotoka kwamba unahitaji kusoma tu sehemu ambayo watu wengi wanaiita Agano Jipya. Kumbuka, “andiko lote limeongozwa na roho ya Mungu nalo ni lenye faida.”—2 Timotheo 3:16.

Njia moja nzuri ya kusoma Biblia ni kuichunguza kichwa kimoja baada ya kingine. Kwa mfano, kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kinachotumiwa na Mashahidi wa Yehova katika utumishi wao kinatia ndani vichwa kama vile: “Jinsi ya Kufanya Maisha ya Familia Yako Yawe Yenye Furaha,” “Ibada Ambayo Mungu Anakubali,” na “Wafu Wako Wapi?”—Ona sanduku kwenye ukurasa wa 18.

[Sanduku katika ukurasa wa 21]

SOMA BIBLIA KULINGANA NA VICHWA

Uhai ulivyoanza na jinsi mwanadamu alivyotenda dhambi Mwanzo

Jinsi taifa la kale la Israeli lilivyoanza Kutoka hadi Kumbukumbu la Torati

Masimulizi yenye kusisimua Yoshua hadi Esta

Mashairi na nyimbo zinazovutia Ayubu, Zaburi, Wimbo wa Sulemani

Jinsi ya kuishi kwa hekima Methali, Mhubiri

Unabii na mwongozo wa maadili Isaya hadi Malaki na Ufunuo

Maisha na mafunzo ya Yesu Mathayo hadi Yohana

Kuanzishwa na kuenea kwa Ukristo Matendo

Barua kwa makutaniko Waroma hadi Yuda