Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Watoto na Intaneti—Mambo Ambayo Wazazi Wanapaswa Kujua

Watoto na Intaneti—Mambo Ambayo Wazazi Wanapaswa Kujua

Watoto na Intaneti—Mambo Ambayo Wazazi Wanapaswa Kujua

WAKATI fulani ilionekana kwamba ingekuwa salama kutumia Intaneti ikiwa kompyuta ingewekwa mahali palipo wazi. Ilifikiriwa kwamba ukifanya hivyo, haitakuwa rahisi kwa watoto wako kufungua vituo hatari au visivyofaa. Bado wazo hilo linafaa, kwa kuwa si jambo linalopatana na akili kuwaruhusu watoto kutumia Intaneti katika chumba chao cha kulala. Lakini, mengi zaidi yanahitajika ili kuwalinda watoto. Siku hizi watoto wanaweza kutumia Intaneti mahali popote kama vile katika maduka yenye huduma za Intaneti (Internet café), kwenye simu za mkononi na vifaa vingine kama hivyo, au kwenye nyumba ya rafiki. Kwa sababu kuna sehemu hizo zote za kutumia Intaneti, ni rahisi kuona jinsi inavyoweza kuwa vigumu kwa mzazi kujua kwamba mtoto wake anatumia Intaneti.

Fikiria baadhi ya mambo ambayo vijana wanafanya kwenye Intaneti na hatari zake.

BARUA PEPE

Ni nini? Ni ujumbe ulioandikwa unaotumwa kupitia kompyuta.

Kwa nini inavutia? Barua pepe ni njia ya haraka na isiyo ghali ya kuwasiliana na marafiki na watu wa familia.

Unachopaswa kujua. Mbali na kuudhi, barua usizotaka zinaweza kuwa na madhara. Mara nyingi zina habari zinazogusia au kutaja moja kwa moja mambo machafu. Anwani nyingine za ziada zinaweza kumwomba mtumiaji, kutia ndani mtoto asiyejua, atoe habari za kibinafsi ambazo zinaweza kufanya utambulisho wake uibiwe. Kujibu barua hizo, hata ikiwa unatuma ujumbe unaosema usitumiwe barua hizo, kutathibitisha kwamba anwani hiyo inatumiwa, na hilo linaweza kufanya utumiwe barua zaidi.

TOVUTI

Ni nini? Ni kurasa za kompyuta ambazo zimetengenezwa na mashirika, taasisi za elimu, biashara, na watu mmoja-mmoja.

Kwa nini zinavutia? Kuna mamilioni ya tovuti zinazowawezesha vijana kununua vitu, kufanya utafiti, kuwasiliana na marafiki, na kucheza au kunakili michezo na muziki.

Unachopaswa kujua. Tovuti zimetumiwa vibaya na watu wasio na nia nzuri. Vituo vingi vinaonyesha watu wakifanya ngono, na ni rahisi kwa watu wasio makini kuvifungua bila kukusudia. Kwa mfano, nchini Marekani uchunguzi uliofanyiwa vijana walio kati ya umri wa miaka 8 na 16 ulionyesha kwamba asilimia 90 ya vijana hao walipata bila kukusudia ponografia (picha au habari za ngono) kwenye Intaneti, mara nyingi walipokuwa wakifanya kazi za shule!

Pia Intaneti inafanya iwe rahisi kufungua tovuti ambazo vijana wanaweza kucheza kamari. Katika uchunguzi uliofanywa nchini Kanada, mvulana 1 kati ya 4 hivi katika kidato cha pili na cha tatu alikiri kwamba amefungua tovuti kama hizo, na wataalamu wana wasiwasi kwa sababu kucheza kamari kwenye kompyuta kunaweza kumfanya mtu awe mraibu sugu. Pia kuna tovuti ambazo zinaunga mkono “kujinyima chakula.” * Vilevile, tovuti za kueneza chuki zinalenga vikundi vya watu wa dini na kabila ndogo-ndogo. Tovuti nyingine zinafundisha jinsi ya kutengeneza mabomu, sumu, na kutekeleza ugaidi. Michezo mingi ya kompyuta inaonyesha jeuri inayopita kiasi na umwagaji mwingi wa damu.

VITUO VYA MAONGEZI

Ni nini? Ni vituo fulani kwenye Intaneti ambavyo watu wanaweza kuwa na mazungumzo ya wakati uleule kupitia kuandikiana kuhusu habari fulani hususa.

Kwa nini vinavutia? Mtoto wako anaweza kuwasiliana na watu wengi walio na mapendezi sawa ambao huenda hajawahi kukutana nao.

Unachopaswa kujua. Mara nyingi, watu wanaowatendea watoto vibaya kingono wanatumia vituo hivyo wakitumaini kumshawishi mtoto afanye naye ngono kwenye Intaneti au hata wakutane ili wafanye ngono. Hebu fikiria mambo yaliyotokea mwandishi mmoja wa kitabu What in the World Are Your Kids Doing Online? alipokuwa akifanya uchunguzi kuhusu usalama wa Intaneti. Mwanamke huyo alijifanya kuwa ana umri wa miaka 12. Kitabu hicho kinasema hivi: “Mara moja mtu fulani alimwomba awasiliane naye kwenye kituo cha maongezi cha faragha. Mwanamke huyo alidai kwamba hajui kufungua kituo hicho, na rafiki yake mpya alimweleza jinsi ya kukifungua. Kisha mtu huyo alimwuliza ikiwa angependa kufanya ngono naye [kwenye Intaneti].”

UJUMBE MFUPI

Ni nini? Ni mawasiliano ya moja kwa moja kati ya watu wawili au zaidi kupitia ujumbe ulioandikwa.

Kwa nini unavutia? Njia hii ya mawasiliano humwezesha mtu kuchagua marafiki atakaowasiliana nao walio katika orodha yake. Hivyo, haishangazi kwamba uchunguzi uliofanywa nchini Kanada unaripoti kwamba asilimia 84 ya vijana walio na umri wa kati ya miaka 16 na 17 wanawatumia marafiki wao ujumbe mfupi na wao hufanya hivyo kwa zaidi ya saa moja kila siku.

Unachopaswa kujua. Ujumbe mfupi unaweza kukengeusha mtoto wako ikiwa anapaswa kuwa akisoma au kufanya jambo linalohitaji awe makini. Kwa kuongezea, unawezaje kuwa na hakika kuhusu mtu ambaye mwana au binti yako anawasiliana naye? Kwa kweli, huwezi kusikiliza mazungumzo hayo.

BLOGU

Ni nini? Ni vitabu vya kuandika mambo ya kibinafsi kwenye Intaneti.

Kwa nini zinavutia? Blogu huwapa vijana nafasi ya kuandika mawazo yao, mapendezi na mambo wanayofanya. Blogu nyingi zinawaruhusu wasomaji waandike maelezo yao na watoto wengi wanafurahi wanapopata kwamba mtu fulani ameandika maelezo yake.

Unachopaswa kujua. Habari zilizo kwenye blogu zinaweza kusomwa na mtu yeyote. Baadhi ya vijana hutoa bila kujali habari zinazoweza kutumiwa kutambulisha familia yao, shule, au mahali wanapoishi. Pia, blogu zinaweza kutumiwa kuchafua majina ya watu, kutia ndani kumharibia sifa mwenye blogu hiyo. Kwa mfano, baadhi ya waajiri hufungua blogu ya mtu aliyeomba kazi wanapochunguza ikiwa wanaweza kumwajiri mtu huyo.

VITUO VYA MAWASILIANO

Ni nini? Ni vituo ambavyo vinawaruhusu vijana watengeneze tovuti zao na kuziboresha kwa kutumia picha, video, na blogu.

Kwa nini vinavutia? Kuanzisha na kuboresha kituo chake kunamwezesha kijana ajitambulishe. Vituo vya mawasiliano vinawaruhusu vijana kukutana na “marafiki” wengi wapya.

Unachopaswa kujua. “Kituo cha mawasiliano ni kama sherehe kwenye Intaneti,” anasema msichana anayeitwa Joanna. “Watu wenye kutisha wanaweza kuwasiliana nawe.” Habari za kibinafsi zinazowekwa kwenye vituo vya mawasiliano zinaweza kutumiwa vibaya na vijana na watu wazima wenye nia mbaya. Kwa hiyo, Parry Aftab, mtaalamu wa usalama kwenye Intaneti anaviita vituo hivyo “duka kubwa kwa ajili ya watu wanaowavizia watoto ili wafanye ngono nao.”

Zaidi ya hilo, urafiki kwenye Intaneti ni wa kijuu-juu tu. Vijana fulani wanakusanya majina ya watu ambao hawajakutana nao uso kwa uso ili waonekane kuwa maarufu na watu wanaotembelea vituo vyao. Katika kitabu chake Generation MySpace, Candice Kelsey anaandika kwamba “ubora wa mtu unaamuliwa na idadi ya watu wanaompenda.” Anaongeza hivi: “Kuamua ubora wa mtu kupitia idadi ya watu wanaompenda kunawafanya watoto wetu wakose utu na kunawashinikiza sana wajitambulishe kwa njia itakayowaletea marafiki wengi zaidi.” Kwa hiyo, kitabu What in the World Are Your Kids Doing Online? kinauliza swali hili muhimu: “Unaweza kuwafundisha watoto jinsi gani wawe na hisia-mwenzi na huruma huku kompyuta ikiwaruhusu kukutana na watu na kuwaacha bila kujali?”

Mifano hiyo sita ni baadhi ya mambo yanayowavutia vijana kutumia Intaneti. Ikiwa wewe ni mzazi unaweza kufanya nini ili kuwalinda watoto wako kutokana na hatari za Intaneti?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Tovuti na mashirika mengi yanayounga mkono kujinyima chakula yanadai kwamba hayafanyi hivyo. Hata hivyo, baadhi yao yanaonyesha kwamba kujinyima chakula si ugonjwa bali ni uamuzi wa mtu. Tovuti kama hizo zina habari kuhusu jinsi ya kuficha uzito wa mwili na jinsi ya kuwaficha wazazi wasijue kwamba kijana hali vizuri.

[Blabu katika ukurasa wa 4]

Huko India watu wanaotumia Intaneti waliongezeka kwa asilimia 54 hivi katika mwaka mmoja, na wengi wa watumiaji hao ni vijana

[Blabu katika ukurasa wa 7]

“Mzazi anaweza kuona kamera iliyounganishwa na kompyuta kuwa njia rahisi na isiyo ya bei ghali kwa mtoto kuwasiliana na marafiki au watu wa ukoo, lakini mtu anayewatendea watoto vibaya kingono anaiona kuwa nafasi ya kuingia kwenye chumba cha kulala cha mtoto wako.”—Robert S. Mueller III, msimamizi wa Shirika la Upelelezi la Marekani (FBI)