Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mtu Anahisije Anaposhuka Moyo?

Mtu Anahisije Anaposhuka Moyo?

Mtu Anahisije Anaposhuka Moyo?

“NILIPOKUWA na umri wa miaka 12,” anakumbuka James, * “niliamka na kuketi kitandani, na nikajiuliza hivi, ‘Je, leo ndiyo siku yangu ya kufa?’” James alikuwa ameshuka moyo sana. James anasema hivi miaka 30 baadaye: “Kila siku maishani mwangu nimepambana na ugonjwa huu wa kihisia na kiakili.” Alipokuwa mtoto, James alihisi kwamba yeye hakuwa mtu wa maana kabisa hata akararua picha zake za utotoni. “Sikudhani nilikuwa mtu wa maana hivi kwamba nikumbukwe,” anasema.

Kwa sababu sisi sote huhisi tumehuzunika mara kwa mara, tunaweza kukata kauli kwamba tunaelewa jinsi mtu aliyeshuka moyo anavyohisi. Lakini mtu aliye na ugonjwa wa kushuka moyo sana anahisije?

Mgeni Asiyetakikana

Tofauti na huzuni ya muda, mara nyingi ugonjwa wa kushuka moyo sana unamzuia mtu asifanye shughuli zake za kila siku.

Kwa mfano, kwa zaidi ya miaka 40, Álvaro amekumbwa na “woga, kuchanganyikiwa kiakili, kuhangaika, na huzuni nyingi.” Anasema hivi: “Kwa sababu ya kushuka moyo, niliathiriwa sana na maoni ya wengine. Kila mara nilijihisi mwenye hatia mambo yalipoenda mrama.” Anaeleza kwamba kushuka moyo ni kama “kuwa na maumivu makali bila kujua maumivu hayo yanatoka wapi, kuwa na hofu bila kujua ni kwa nini na, jambo baya hata zaidi, kutotaka hata kidogo kuzungumzia hali yako.” Hata hivyo, sasa amepata kitulizo. Amejua chanzo cha tatizo lake. Anasema, “Kujua kwamba wengine pia wanakabili tatizo kama langu kumenifanya nijihisi vizuri.”

Nchini Brazili, Maria mwenye umri wa miaka 49 anasema kwamba kushuka moyo kulimfanya akose usingizi, apatwe na maumivu, audhike, na awe na “huzuni isiyoisha.” Maria alipata kitulizo ugonjwa wake ulipogunduliwa. “Lakini nikaanza kuwa na wasiwasi,” anasema, “kwa sababu ni watu wachache sana wanaoelewa ugonjwa huo, na unaonwa kuwa wenye kuaibisha.”

Je, Kuna Sababu ya Kuhuzunika?

Ingawa nyakati nyingine inakuwa rahisi kujua ni nini kinachokufanya ushuke moyo, mara nyingi ugonjwa huo huja bila kutarajiwa. “Ghafula maisha yako yanafunikwa na wingu la huzuni bila sababu yoyote,” anaeleza Richard kutoka Afrika Kusini. “Hakuna mtu unayemjua ambaye amekufa, na hakuna jambo lolote lenye kuhuzunisha limetukia. Hata hivyo, unajihisi ukiwa mchovu na umehuzunika. Na hakuna chochote kinachoweza kuondoa wingu hilo. Unakata tamaa kabisa na hujui ni kwa nini.”

Kushuka moyo si ugonjwa wa kuaibikia. Hata hivyo, Ana anayeishi Brazili aliaibika ilipogunduliwa anaugua ugonjwa wa kushuka moyo. “Hata sasa, miaka minane baadaye bado ninaaibika,” anasema. Anashindwa hasa kukabiliana na hisia za kuhuzunika sana. Anaeleza hivi: “Nyakati nyingine ninateseka sana hivi kwamba ninahisi maumivu. Misuli yangu yote huuma.” Nyakati hizo inakuwa vigumu kutoka kitandani. Kisha kuna pindi Ana hulia mfululizo. Anasema, “Mimi hulia mpaka ninahisi uchovu, ni kana kwamba damu imeacha kuzunguka mwilini.”

Biblia inakubali kwamba mtu anaweza kushuka moyo sana. Kwa mfano, mtume Paulo alihangaika kwamba mtu mmoja ‘angemezwa na huzuni yake ya kupita kiasi [‘angezama katika uchungu mwingi mno,’ Verbum Bible].’ (2 Wakorintho 2:7) Watu fulani hufadhaika sana hivi kwamba wanaona ni afadhali wafe. Wengi huhisi kama nabii Yona aliyesema: “Ni afadhali mimi nife kuliko niwe hai.”—Yona 4:3.

Watu walioshuka moyo wanaweza kufanya nini ili kukabiliana na ugonjwa huo wenye kufadhaisha?

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 2 Majina katika makala hizi yamebadilishwa.

[Blabu katika ukurasa wa 3]

“Ghafula maisha yako yanafunikwa na wingu la huzuni bila sababu yoyote”