Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Siri ya 3: Kushirikiana

Siri ya 3: Kushirikiana

Siri ya 3: Kushirikiana

“Wawili ni afadhali kuliko mmoja . . . Mmoja wao akianguka, yule mwingine anaweza kumwinua mwenzake.”—Mhubiri 4:9, 10.

Hilo linahusisha nini? Wenzi wa ndoa wenye mafanikio huheshimu mpango wa Mungu wa ukichwa unaotajwa katika Biblia. (Waefeso 5:22-24) Isitoshe, mume na mke hutumia maneno kama vile “yetu” na “sisi” badala ya “yangu” na “mimi.” Kunapokuwa na ushirikiano, mume na mke hawajifikirii tena kuwa waseja. Wao ni “mwili mmoja,” maneno ambayo Biblia inatumia kuonyesha uhusiano wa karibu na wenye kudumu wa ndoa.—Mwanzo 2:24.

Kwa nini ni muhimu? Ikiwa wewe na mwenzi wako hamshirikiani, mambo madogo yanaweza kuwa makubwa huku kila mmoja akimshambulia mwenzake badala ya kushughulikia tatizo linalowakabili. Lakini ikiwa wewe na mwenzi wako mnashirikiana, mnakuwa kama marubani wawili wanaoshirikiana kuendesha ndege ileile badala ya marubani wawili walio katika ndege mbili tofauti zilizo karibu kugongana. Mnapokosa kuelewana, mnatafuta masuluhisho yanayofaa badala ya kupoteza wakati na nguvu za kihisia kwa kulaumiana na kushtakiana.

Jaribu kufanya hivi. Jaribu kupima unashirikiana kadiri gani na mwenzi wako kwa kutumia maswali yafuatayo.

Je, mimi huona pesa ninazochuma kuwa “zangu,” kwa kuwa mimi ndiye niliyezichuma?

Je, mimi hujitenga na watu wa ukoo wa mwenzi wangu, hata ingawa yeye ana uhusiano wa karibu nao?

Ili nipumzike kabisa, je, mimi huhitaji kujitenga na mwenzi wangu?

Azimia. Fikiria njia moja au mbili ambazo unaweza kuonyesha kuwa unashirikiana na mwenzi wako.

Mbona usimwulize mwenzi wako madokezo?

[Picha katika ukurasa wa 5]

Kushirikiana kunamaanisha ninyi ni marubani wawili wanaoshirikiana kuendesha ndege ileile