Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Uwapongeze Wengine?

Kwa Nini Uwapongeze Wengine?

Maoni Ya Biblia

Kwa Nini Uwapongeze Wengine?

WATU wengi huhisi kwamba jitihada zao hazitambuliwi na wengine. Kwa mfano, mara nyingi wafanyakazi huhisi kwamba hawathaminiwi na waajiri wao. Wenzi wengi wa ndoa husema kwamba hawathaminiwi na wenzi wao. Na watoto fulani hufikiri kwamba hawawezi kutimiza matarajio ya wazazi wao. Kwa kweli, hisia hizo zinaweza kuepukwa ikiwa sisi sote tutajitahidi kuwapongeza wengine mara kwa mara.

Katika ulimwengu wa leo, si jambo la kawaida kwa mtu kumpongeza mwingine kwa unyoofu. Hilo halishangazi kwa kuwa Biblia ilitabiri hivi: “Katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, . . . wasio na shukrani, wasio washikamanifu.”​—2 Timotheo 3:1, 2.

Je, umewahi kupongezwa kutoka moyoni? Basi unajua jinsi hilo huchangamsha na kumtia mtu moyo. “Neno linalosemwa wakati unaofaa ni jema kama nini!” inasema Biblia. (Methali 15:23) Maandiko Matakatifu yanaweza kutusaidia kuwatendea wengine kwa fadhili.

Tafuta Sifa Nzuri za Wengine

Kwa kuwa Mungu anapendezwa sana nasi, yeye huona na kuthamini sifa zetu nzuri na matendo yetu mema. Biblia inatuhakikishia hivi: “Macho yake [Mungu] yanaenda huku na huku duniani kote ili aonyeshe nguvu zake kwa ajili ya wale ambao moyo wao ni mkamilifu kumwelekea yeye.” (2 Mambo ya Nyakati 16:9) Tunapoonyesha upendo wetu kwa Mungu kwa kutii sheria zake, bila shaka yeye ataona jambo hilo.

Yehova Mungu hatafuti kasoro zetu. Ikiwa angefanya hivyo, hakuna hata mmoja wetu ambaye angeweza kusimama. (Zaburi 130:3) Badala yake, Yehova ni kama mchimbaji wa migodi ambaye hutafuta-tafuta kwa subira mawe yenye thamani katika rundo la mawe. Mchimbaji huyo anapopata jiwe lenye thamani, yeye hushangilia. Huenda kwa nje jiwe hilo lisionekane kuwa lenye thamani, lakini mchimbaji ndiye anayejua thamani yake. Vivyo hivyo, Mungu anapochunguza moyo wetu, yeye hutafuta sifa nzuri, si kasoro. Anapopata sifa hizo, anashangilia. Anajua kwamba sifa hizo zikiboreshwa, zinaweza kutokeza kitu chenye thamani kwelikweli, yaani, mwabudu wa Yehova aliye mwaminifu na aliyejitoa.

Tunaweza kujifunza kutokana na mfano wa Mungu. Tunapowatazama wengine, huenda tukashawishiwa kukazia fikira kasoro zao. Lakini tukiwaona watu jinsi Yehova anavyowaona, tutatafuta sifa zao nzuri. (Zaburi 103:8-11, 17, 18) Tunapopata sifa hizo nzuri, tuwapongeze. Kutakuwa na matokeo gani? Bila shaka maneno yetu yatawaburudisha, nao watajitahidi zaidi kufanya yaliyo sawa! Sisi tutapata shangwe inayotokana na kutoa.​—Matendo 20:35.

Tambua Matendo Mema

Yesu alitambua na kuona matendo mema ya wengine. Pindi moja, mwanamke mmoja mgonjwa aliyekuwa na woga alipogusa mavazi yake ya nje ili aponywe, Yesu alimpongeza na kumwambia: “Binti yangu, imani yako imekuponya.”​—Marko 5:34.

Katika pindi nyingine, Yesu alipokuwa akifundisha katika hekalu huko Yerusalemu, aliwaona watu wengi matajiri wakitumbukiza pesa ndani ya masanduku ya hazina. Kisha akamwona mjane fulani mwenye uhitaji “akitumbukiza humo sarafu ndogo mbili za thamani ndogo sana.” Wengine walikuwa wametoa mchango wa pesa nyingi kuliko mjane huyo. Hata hivyo, Yesu alimpongeza mjane huyo hadharani kwa sababu ya unyoofu wake kwa kusema: “Ninawaambia ninyi kwa kweli, Mjane huyu, ijapokuwa ni maskini, ametumbukiza ndani zaidi kuliko hao wote. Kwa maana wote hawa walitumbukiza zawadi kutokana na ziada yao, lakini mwanamke huyu kutokana na uhitaji wake alitumbukiza ndani riziki yote aliyokuwa nayo.”​—Luka 21:1-4.

Tunaweza kumwigaje Yesu? Biblia inasema: “Usiwanyime watu mema wanayostahili, mkono wako ukiwa na uwezo wa kuyafanya.”​—Methali 3:27.

Pongezi Ina Nguvu

Katika ulimwengu wa leo usio na shukrani, sote tunahitaji kuhisi kwamba tunathaminiwa na kupendwa. Tunapowapongeza wengine kwa unyoofu, tunawaimarisha na kuwatia moyo. Pongezi zetu za kutoka moyoni huwachochea kuendelea kufanya yote wawezayo.​—Methali 31:28, 29.

Biblia inawahimiza Wakristo wote hivi: “Acheni tufikiriane ili kuchocheana katika upendo na matendo mazuri.” (Waebrania 10:24) Ulimwengu ungekuwa mahali tofauti kabisa ikiwa kila mtu angependezwa kikweli na wengine, ikiwa angetafuta sifa zao nzuri, na kutambua matendo yao mema. Kwa kweli, pongezi ina nguvu!

JE, UMEJIULIZA HIVI?

● Kwa nini tuwapongeze wengine kwa sababu ya matendo yao mema?​—Methali 15:23.

● Yehova anapotuchunguza, yeye hutafuta nini?​—2 Mambo ya Nyakati 16:9.

● Tunapaswa kuwapongeza wengine wakati gani?​—Methali 3:27.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Je, wewe huona na kutambua matendo mema ya wengine?