Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ninawi lilikuwa jiji lenye majengo na minara mikubwa ya ukumbusho

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Ni nini kilicholipata jiji la Ninawi baada ya siku za Yona?

BLOGU ya Jumba la Makumbusho la Uingereza iliripoti kwamba kufikia karne ya saba K.W.K., Ashuru ilikuwa milki kubwa zaidi ya ulimwengu, “ikianzia Kipro kwa upande wa magharibi hadi Iran kwa upande wa mashariki, na pindi fulani hata ilitia ndani Misri.” Ninawi, jiji lake kuu, lilikuwa jiji kubwa zaidi duniani. Lilikuwa na minara mikubwa ya ukumbusho, bustani maridadi, makasri ya kifahari, na maktaba kubwa. Maandishi ya ukutani katika jiji la kale la Ninawi yanaonyesha kwamba Mfalme Ashurbanipali, kama wafalme wengine wa Ashuru, alijiita “mfalme wa ulimwengu.” Wakati huo, ilionekana kana kwamba hakuna ambaye angeweza kuishinda Ashuru na Ninawi.

Serikali Kuu ya Ulimwengu ya Ashuru ilikuwa milki kuu zaidi ulimwenguni wakati huo

Hata hivyo, Ashuru ilipokuwa imefikia kilele cha mafanikio, Sefania, nabii wa Yehova, alitabiri hivi: “[Yehova] . . . [ataangamiza] Ashuru, naye atalifanya Ninawi liwe ukiwa, liwe kavu kama jangwa.” Pia, Nahumu, nabii wa Yehova, alitabiri hivi: “Poreni fedha, poreni dhahabu! . . . Jiji liko tupu, liko ukiwa, na limeharibiwa kabisa! . . . Kila mtu atakayekuona atakukimbia na kusema, ‘Jiji la Ninawi limeangamizwa!’” (Sef. 2:13; Nah. 2:9, 10; 3:7) Watu waliposikia unabii huo, huenda walijiuliza hivi: ‘Je, kweli hilo linawezekana? Je, kweli Ashuru yenye nguvu inaweza kushindwa?’ Ni lazima lilionekana kuwa jambo lisilowezekana.

Ninawi likawa jiji lililoachwa ukiwa!

Hata hivyo, lile ambalo halikudhaniwa lilitukia! Kufikia mwishoni mwa karne ya saba K.W.K., Ashuru ilikuwa imeshindwa na Wababiloni na Wamedi. Hatimaye, Ninawi liliachwa ukiwa na kusahaulika! Chapisho lililotolewa na Jumba la Makumbusho ya Sanaa la Jijini New York, lilisema hivi: “Kufikia zile Enzi za Kati, eneo hilo lilikuwa limeachwa ukiwa na kufukiwa, na Ninawi ilikumbukwa tu kupitia Biblia.” Kulingana na Hifadhi ya Mtandaoni ya Biblical Archaeology Society, kufikia mwanzoni mwa miaka ya 1800, “hakuna hata aliyekuwa anajua ikiwa jiji kuu la Ashuru liliwahi kuwepo.” Lakini mwaka wa 1845, mvumbuzi wa vitu vya kale, Austen Henry Layard, alianza kuchimbua eneo la jiji la Ninawi. Magofu yaliyogunduliwa yalithibitisha utukufu wa kale wa jiji la Ninawi.

Kutimia kwa usahihi kwa unabii mbalimbali kuhusu Ninawi kunaimarisha uhakika wetu kwamba unabii wa Biblia kuhusu mwisho wa serikali kuu za leo utatimia pia.​—Dan. 2:44; Ufu. 19:15, 19-21.