Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Ni Jambo Gani Hasa Linaloamua Jinsi Maisha Yako Yatakavyokuwa?

Ni Jambo Gani Hasa Linaloamua Jinsi Maisha Yako Yatakavyokuwa?

Watu wengi wanaamini kwamba wakati wao ujao unaongozwa na nguvu fulani zisizoonekana. Kwa sababu ya imani hiyo, wanafuata desturi ambazo wanahisi zitaboresha maisha yao.

MAMBO AMBAYO WATU WENGI WANAAMINI

UNAJIMU: Baadhi ya watu wanaamini kwamba wakati wao ujao unategemea jinsi nyota zilivyojipanga katika siku waliyozaliwa. Wanafanya uaguzi au kuangalia utabiri wa nyota ili kujua mambo yatakayowapata wakati ujao na kisha wanafanya mambo yatakayowaepusha na hatari au yatakayowasaidia kupata mafanikio.

FENG SHUI: Wengine wanaamini ili wafanikiwe, wanahitaji kuhakikisha kwamba mazingira yao hayapingani na nguvu fulani zisizoonekana zinazowazunguka. Lo Wing, * anayeishi Hong Kong, anasema, “Mbashiri wa feng shui aliniambia kwamba nikiweka jiwe fulani linalofanana na kioo kwenye sehemu hususa ya duka langu, lingeweza kunisaidia kupata pesa nyingi zaidi.”

IBADA YA MABABU WALIOKUFA: Watu wengine wanaamini kwamba wanapaswa kuwapendeza mababu zao waliokufa au miungu mbalimbali ili walindwe na kupata baraka. Van, anayeishi Vietnam, anasema, “Niliamini kwamba kuwaonyesha heshima mababu zangu waliokufa kungenisaidia mimi na watoto wangu kuwa na maisha bora sasa na wakati ujao.”

KUZALIWA UPYA KATIKA MWILI MWINGINE: Watu wengi wanaamini kwamba maisha ni mzunguko usiokuwa na mwisho unaohusisha kuwa hai, kufa, na kuzaliwa upya. Wanaamini kwamba mambo mazuri au mabaya wanayokabili sasa ni matokeo ya mambo waliyofanya katika maisha yao ya awali.

Hata hivyo, wengi wanaamini kwamba mambo hayo ni imani za ushirikina. Lakini, watu haohao wanafanya mambo kama vile kusoma viganja vya mikono, kuangalia utabiri wa nyota, kupiga ramli, na kadhalika. Wanahisi kwamba mazoea hayo yanaweza kuwasaidia kujua wakati wao ujao.

MATOKEO NI NINI?

Je, wale wanaotegemea imani na mazoea hayo wamefanikiwa na kupata tumaini la kuwa na maisha bora ya wakati ujao?

Fikiria kisa cha Hào, anayeishi Vietnam. Alitumia unajimu, feng shui, na kuabudu mababu ili apate mwongozo maishani. Je, alifanikiwa? Hào anasema, “Biashara yangu ilifilisika, nilikuwa na madeni mengi, migogoro ya familia, na nilikuwa na hali mbaya kihisia.”

Qiuming, kutoka Taiwan, aliamini pia unajimu, kuzaliwa upya katika mwili mwingine, majaliwa, feng shui, na kuabudu mababu waliokufa. Baada ya kuchunguza kwa makini imani hizo, alisema: “Niligundua kwamba mafundisho na mazoea hayo yanapingana na yanachanganya sana. Nilitambua kwamba, mara nyingi ubashiri wa nyota si sahihi. Na kuhusu imani ya kuzaliwa upya katika mwili mwingine, nilijiuliza, ikiwa hukumbuki maisha yako ya awali, unawezaje kubadili maisha yako ya sasa, na kuboresha maisha ya wakati ujao?”

“Niligundua kwamba mafundisho na mazoea hayo yanapingana na yanachanganya sana.”​—QIUMING, TAIWAN

Hào, Qiuming, na watu wengine wengi wametambua ukweli kwamba, wakati wao ujao hautegemei majaliwa, nyota, mababu waliokufa, au kuzaliwa upya katika mwili mwingine. Lakini je, hilo linamaanisha kwamba hatuwezi kuboresha maisha yetu ya wakati ujao?

Watu wengi wanahisi kwamba njia nzuri ya kupata maisha bora ya wakati ujao ni kufuatilia elimu ya juu zaidi na utajiri. Baadhi ya wale waliofanya uamuzi huo wamepata matokeo gani?

^ fu. 5 Baadhi ya majina yamebadilishwa katika makala hii na inayofuata.

^ fu. 16 Maneno hayo yanapatikana katika Biblia Takatifu kwenye Wagalatia 6:7. Wazo hilo pia huonyeshwa katika misemo maarufu ya watu wa Mashariki kama vile, Ukipanda matikiti maji, utavuna matikiti maji; ukipanda maharagwe utavuna maharagwe.