Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tumia kwa Hekima Hali Zenye Kubadilika Maishani

Tumia kwa Hekima Hali Zenye Kubadilika Maishani

Tumia kwa Hekima Hali Zenye Kubadilika Maishani

Pum, Jan, Dries, na Otto ni wazee wanne Wakristo wanaoishi Uholanzi ambao hali zao zinafanana. Wote wanne wamefunga ndoa na wana watoto. Zaidi ya hayo, miaka kadhaa iliyopita, wote walikuwa wakifanya kazi za kuajiriwa na waliishi katika nyumba nzuri. Hata hivyo, wote waliacha kazi na kuanza kutumia wakati na nguvu zao zote kuendeleza mambo ya Ufalme. Ni nini kilichowawezesha kufanya mabadiliko hayo? Wote wanne walitumia ifaavyo hali zao zilizobadilika maishani.

HATIMAYE hali za kila mmoja wetu zitabadilika kwa njia moja au nyingine. Mabadiliko mengi kama vile kufunga ndoa, kupata watoto, au kutunza wazazi waliozeeka huongeza majukumu yetu. Hata hivyo, mabadiliko mengine hutupatia uhuru zaidi wa kupanua huduma yetu ya Kikristo. (Mathayo 9:37, 38) Kwa mfano, huenda watoto wetu ambao ni watu wazima wakaondoka nyumbani, au huenda tukastaafu.

Isitoshe, hata ingawa huenda hali zetu zikabadilika iwe tunataka au hatutaki, Wakristo wengine wamefanya mabadiliko maishani mwao ili kupanua huduma yao. Hivyo ndivyo Pum, Jan, Dries, na Otto walivyofanya. Jinsi gani?

Watoto Wanapoondoka Nyumbani

Pum alifanya kazi ya kuweka hesabu katika kampuni moja ya madawa. Mara nyingi, yeye na mke wake Anny, pamoja na binti zao wawili, walitumikia wakiwa mapainia-wasaidizi. Pum na Anny walipanga kuwa na tafrija pamoja na mapainia wengine. Wanasema: “Jambo hilo lilituepusha na matatizo ambayo tungepata kama tungeshirikiana na watu wengine.” Kwa kuchochewa na kielelezo cha wazazi wao, binti hao wawili walianza upainia wa kawaida baada ya kumaliza shule ya sekondari.

Watoto wao walipoondoka nyumbani, Pum na Anny waliona kwamba hali zao zimebadilika na wana uhuru zaidi na pesa za kusafiri sehemu mbalimbali zenye kuvutia au kufurahia tafrija nyinginezo. Hata hivyo, Pum na Anny waliamua kutumia hali hizo zilizobadilika ili kupanua huduma yao ya Kikristo. Kwa hiyo, Pum akamwomba mwajiri wake ruhusa ili asiwe akifanya kazi siku moja kwa juma. Baadaye, Pum alifanya mipango iliyomwezesha kuanza kazi saa 1:00 asubuhi na kuondoka saa 8:00 alasiri. Bila shaka, kupunguza muda wa kufanya kazi kulimaanisha kukabili magumu ya kuishi kwa mshahara mdogo. Hata hivyo, walifaulu na mnamo mwaka wa 1991, Pum akajiunga na mke wake katika upainia wa kawaida.

Kisha, Pum akaombwa awe mtunzaji-msaidizi wa Jumba la Kusanyiko la Mashahidi wa Yehova. Ombi hilo lilimaanisha kwamba wenzi hao wa ndoa wangeacha makao yao walimoishi kwa miaka 30 na kuhamia nyumba iliyokuwa kwenye uwanja wa Jumba la Kusanyiko. Nao wakafanya hivyo. Je, ilikuwa vigumu? Anny anajibu kwamba alipoanza kutamani kurudi nyumbani, alijiuliza, ‘Je, mimi ni kama mke wa Loti?’ Alikataa ‘kutazama nyuma.’—Mwanzo 19:26; Luka 17:32.

Pum na Anny wanaona kwamba wamepata baraka tele kwa sababu ya uamuzi wao. Kati ya mambo mengi ambayo wanafurahia ni utumishi wao kwenye Jumba la Kusanyiko, kutayarisha makusanyiko ya wilaya na kuwasiliana na waangalizi (wahudumu wasafirio) ambao hutoa hotuba kwenye jumba hilo. Mara kwa mara wao hutembelea makutaniko mbalimbali wakati Pum anapotumikia akiwa mwangalizi wa mzunguko wa badala.

Ni nini kilichowasaidia ndugu hao na wake zao wapanue utumishi wao? Pum anasema: “Kunapokuwa na badiliko kubwa maishani mwako, inakupasa uazimie kutumia hali hizo mpya ifaavyo zaidi.”

Kufanya Maisha Yawe Sahili

Jan na mke wake Woth wana watoto watatu. Kama Pum na familia yake, Jan naye alitumia kwa hekima hali zilizobadilika. Kwa miaka mingi Jan alifanya kazi yenye mshahara mnono kwenye benki na familia yake iliishi maisha ya starehe. Hata hivyo, alikuwa akitamani sana kupanua huduma yake. Anaeleza: “Nilianza kuthamini kweli maishani mwangu, na upendo wangu kwa Yehova ukaongezeka.” Kwa hiyo mnamo mwaka wa 1986, Jan alibadili hali zake. Anasema: “Kazi ilipopangwa upya ofisini, nilipunguza saa nilizofanya kazi. Wafanyakazi wenzangu walishangaa na kunibandika jina Diwodo kwa sababu nilifanya kazi siku ya dinsdag [Jumanne], woensdag [Jumatano], na donderdag [Alhamisi]. Mshahara wangu ulipungua kwa asilimia 40. Niliuza nyumba yetu na kununua mashua-nyumba ili tuweze kutumikia mahali ambako kulikuwa na uhitaji mkubwa wa watangazaji wa Ufalme. Baadaye, niliamua kustaafu mapema na mshahara wangu ukapungua tena kwa asimilia 20, hata hivyo, mwaka wa 1993 nilianza upainia wa kawaida.”

Leo, Jan ni mshiriki wa Halmashauri ya Uhusiano na Hospitali na mara kwa mara ametumikia akiwa mwangalizi wa kusanyiko. Licha ya afya yake mbaya, Woth hufanya upainia msaidizi mara kwa mara. Sasa watoto wote watatu wamefunga ndoa, nao pamoja na wenzi wao ni wahudumu wenye bidii wa Ufalme.

Jan amefaulu jinsi gani kufanya maisha yake yawe sahili? Anajibu, “Tulipokuwa na pesa nyingi tulikuwa waangalifu tusipende sana vitu vya kimwili. Leo huenda ikawa vigumu kidogo kungoja kwa muda kabla ya kupata kitu fulani tunachohitaji, hata hivyo, baraka za kiroho na mapendeleo ambayo tumepata hujazia uhitaji huo.”

Kama Jan na Woth, Dries na mke wake Jenny waliamua pia kufanya maisha yao yawe sahili ili wapate wakati zaidi wa kushughulikia mambo ya Ufalme. Dries na Jenny walitumikia wakiwa mapainia hadi walipopata mtoto. Kwa hiyo, ili kutunza familia yake, Dries alifanya kazi ya uandishi kwenye kampuni moja kubwa. Waajiri wake walithamini kazi yake na wakataka kumpandisha cheo. Lakini Dries akakataa kwa sababu kama angalikubali angalikuwa na wakati mchache wa kushiriki katika utendaji wa Kikristo.

Dries na Jenny walihitaji kutumia wakati wao mwingi na nguvu ili kulea watoto na pia kumtunza mama ya Jenny aliyekuwa mgonjwa. Hata hivyo, waliendelea kusitawisha roho ya upainia. Ni nini kilichowasaidia kufanya hivyo? Jenny anaeleza: “Tuliishi na mapainia, tuliwaalika kwa chakula, na kuwapa waangalizi wa mzunguko mahali pa kulala.” Dries anaendelea kusema: “Tuliishi maisha sahili na kuepuka kuwa na madeni. Tuliamua kutojihusisha kamwe na biashara kubwa-kubwa au kununua nyumba, ili vitu hivyo visiwe kikwazo baadaye.”

Dries na Jenny walithawabishwa sana kwa uamuzi wao wa kufanya mabadiliko ili waweze kuwa na wakati mwingi zaidi kwa ajili ya mambo ya Ufalme. Sasa wana wao wawili ni wazee wa kutaniko, na pia wanafanya upainia pamoja na wake zao. Dries na Jenny walitumikia wakiwa mapainia wa pekee, na baadaye Jenny akawa anaandamana na mumewe katika kazi ya mzunguko. Sasa wanafanya kazi ya kujitolea Betheli, ambako Dries ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi.

Kustaafu Mapema

Kama Dries na Jenny, Otto na mke wake Judy walipainia kabla ya kupata binti zao wawili. Judy alipokuwa na mimba ya mtoto wao wa kwanza, Otto aliajiriwa kazi ya ualimu.

Watoto wao walipokuwa wakikua, mara nyingi Otto na Judy waliwaalika mapainia nyumbani kwao ili binti zao waweze kuona furaha wanayopata Wakristo ambao ni watumishi wa wakati wote. Baada ya muda, binti yao mkubwa alianza utumishi wa upania. Baadaye, alihudhuria Shule ya Gileadi naye pamoja na mume wake, wanatumikia wakiwa mishonari katika nchi moja ya Afrika. Binti yao mdogo alianza upainia mwaka wa 1987, na Judy akajiunga naye.

Hali zilipobadilika shuleni na Otto akawa anaweza kufanya kazi kwa muda wa saa chache, alitumia muda wa ziada aliopata ili kufanya upainia. Hatimaye aliacha kazi hiyo kabisa. Leo, yeye ni mwangalizi wa mzunguko, naye hutumia ujuzi aliopata alipokuwa mwalimu kuimarisha makutaniko kiroho.

Otto anatoa ushauri gani kwa wale wanaostaafu mapema? “Unapostaafu, usiamue kustarehe kwa mwaka mmoja au zaidi. Ni rahisi kuzoea kustarehe na punde si punde usahau upainia. Badala yake, panua huduma yako bila kukawia.”

Kutumia Vizuri Uzoefu Uliopata Maishani

Ni kweli kwamba ndugu kama Pum, Jan, Dries, na Otto hawana nguvu walizokuwa nazo wakiwa vijana. Lakini wana ukomavu, uzoefu, na hekima zaidi. (Mithali 20:29) Wanaelewa hali za akina baba, na kwa kuwa wameishi na wake zao, wanaelewa kwa kadiri fulani hali za akina mama. Wao pamoja na wake zao wametatua matatizo ya familia na kuwawekea watoto wao miradi ya kiroho. Otto anasema: “Nikiwa mwangalizi wa mzunguko naona kwamba shauri ninalotoa kuhusu familia husaidia kwa kuwa hata mimi nimelea watoto.” Vivyo hivyo, Dries husaidia sana vijana wengi wanaotumika Betheli kwa sababu ya uzoefu aliopata akiwa baba.

Naam, ujuzi wao huwasaidia kushughulikia mahitaji mbalimbali kutanikoni. Uzoefu wao umewanoa watumie nguvu zao kwa njia bora hata zaidi. (Mhubiri 10:10) Kwa kweli, mara nyingi wanaweza kutimiza mengi zaidi ya wale walio na nguvu nyingi lakini wasio na uzoefu.

Ndugu kama hao, pamoja na wake zao, ni vielelezo bora kwa vijana miongoni mwa watu wa Yehova. Vijana huona kwamba ndugu kama hao na wake zao wamepata magumu na baraka nyingi zinazotajwa katika vichapo vyetu vya Kikristo. Ni jambo linalotia moyo kuona wanaume na wanawake wanaodhihirisha roho kama ya Kalebu ambaye, ingawa alikuwa mzee, aliomba mgawo mgumu.—Yoshua 14:10-12.

Igeni Imani Yao

Je, unaweza kuiga imani na hatua walizochukua wenzi hao wa ndoa wanaotajwa katika makala hii? Kumbuka kwamba waliishi kupatana na kweli. Waliwasaidia watoto wao wasitawishe tamaa ya upainia. Jan anasema walifanya hivyo “kwa kuwawekea kielelezo cha kumpenda Yehova na tengenezo lake, kwa kufanya mipango ya kuwa na ushirika ufaao, na kwa kuwazoeza watoto wao waweze kujitegemeza kifedha.” Pia walifanya kazi na kucheza pamoja wakiwa familia. Pum anasema, “Wakati wa likizo, kwa kawaida familia nzima ilihubiri asubuhi na kufurahia tafrija pamoja alasiri.”

Zaidi ya hayo, Wakristo hao walipanga mambo mapema, hivyo hali zao zilipobadilika, walikuwa tayari kuzitumia ifaavyo. Waliweka miradi na kufanya maamuzi yaliyowasaidia kufikia miradi yao kwa haraka zaidi. Walitafuta njia za kupunguza muda waliotumia kazini na walikuwa tayari kuishi kwa mshahara mdogo. (Wafilipi 1:10) Wake zao waliwaunga mkono kabisa. Wote walikuwa na tamaa kubwa ya kuingia kwenye ‘mlango mkubwa uongozao kwenye utendaji’ na hivyo kupata baraka nyingi kutoka kwa Yehova.—1 Wakorintho 16:9; Mithali 10:22.

Je, wewe pia unatamani kupanua huduma yako? Ikiwa ndivyo, basi tumia ifaavyo hali zinazobadilika maishani mwako.

[Picha katika ukurasa wa 20]

Pum na Anny wakitunza Jumba la Kusanyiko

[Picha katika ukurasa wa 20]

Jan na Woth wakihubiri

[Picha katika ukurasa wa 21]

Dries na Jenny wakiwa Betheli

[Picha katika ukurasa wa 21]

Otto na Judy wakijitayarisha kutembelea kutaniko jingine