Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Thamini Ukarimu wa Yehova

Thamini Ukarimu wa Yehova

YEHOVA ni Mungu mkarimu. (Yak. 1:17) Tunaona wazi ukarimu wa Yehova tunapotazama uumbaji wake, kuanzia anga lenye nyota nyingi hadi mimea inayofunika dunia.—Zab. 65:12, 13; 147:7, 8; 148:3, 4.

Mtunga zaburi alithamini sana uumbaji wa Yehova hivi kwamba alichochewa kutunga wimbo ili kumsifu. Soma Zaburi ya 104, ili uone ikiwa una maoni kama yake. Alisema hivi: “Nitamwimbia Yehova katika maisha yangu yote; nitampigia Mungu wangu muziki maadamu nipo.” (Zab. 104:33) Je, ungependa kufanya vivyo hivyo?

MFANO BORA WA UKARIMU

Yehova anataka tuige ukarimu wake. Anatusaidia pia kuelewa umuhimu wa kuwa wakarimu. Alimwongoza mtume Paulo kuandika hivi: “Uwape maagizo wale walio matajiri katika mfumo wa mambo wa sasa wasitake makuu, na waweke tumaini lao, si katika utajiri usio hakika, bali katika Mungu, ambaye hutupa sisi vitu vyote kwa wingi ili tuvifurahie; wafanye mema, wawe matajiri katika matendo mazuri, wawe wakarimu, tayari kushiriki, wakijiwekea wenyewe kwa usalama hazina ya msingi mzuri kwa ajili ya wakati ujao, ili waushike imara uzima ulio wa kweli.”—1 Tim. 6:17-19.

Mtume Paulo alipowaandikia Wakorintho barua yake ya pili, alikazia mtazamo unaofaa kuhusu kutoa. Alisema hivi: “Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” (2 Kor. 9:7) Kisha, Paulo alieleza faida za ukarimu; wapokeaji hunufaika kwa kuwa uhitaji wao unatoshelezwa, na watoaji hufaidika kwa kupokea baraka za kiroho.—2 Kor. 9:11-14.

Paulo alimalizia sehemu ya barua yake kwa kueleza jambo la pekee linalothibitisha kwamba Mungu ni mkarimu sana. Alisema hivi: “Mungu apewe shukrani kwa ajili ya zawadi yake ya bure isiyoelezeka.” (2 Kor. 9:15) Ni wazi kwamba zawadi ya Yehova inahusisha wema wote ambao amewafanyia wanadamu kupitia Yesu Kristo. Zawadi hiyo ni ya pekee sana hivi kwamba hatuwezi kufafanua kikamili thamani yake.

Tunaweza kuonyeshaje kwamba tunathamini mambo yote ambayo Yehova na Mwana wake wametufanyia na yale watakayotufanyia? Njia moja ni kuwa wakarimu kwa kutoa wakati, nguvu, na mali zetu ili kuendeleza masilahi ya ibada safi, iwe michango yetu ni midogo au mikubwa.—1 Nya. 22:14; 29:3-5; Luka 21:1-4.