Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Anatupatia Uhuru wa Kuchagua

Yehova Anatupatia Uhuru wa Kuchagua

Mkaribie Mungu

Yehova Anatupatia Uhuru wa Kuchagua

Kumbukumbu la Torati 30:11-20

“MARA nyingi nimekuwa nikifikiria kwa woga kwamba siwezi kuwa mwaminifu kwa Yehova.” Hivyo ndivyo alivyosema mwanamke mmoja Mkristo ambaye alihisi kwamba mambo mabaya yaliyompata akiwa mtoto yangemfanya ashindwe kuwa mwaminifu. Je, ndivyo ilivyo? Je, ni kweli kwamba hali tulizokabili zinatuzuia kuwa waaminifu kwa Mungu? Hapana. Yehova Mungu ametupatia zawadi ya uhuru wa kuchagua, kwa hiyo tunaweza kujichagulia wenyewe jinsi tutakavyoishi. Yehova anataka tufanye maamuzi yanayofaa, na Neno lake, Biblia, linatuambia jinsi tunavyoweza kufanya hivyo. Fikiria maneno ya Musa, yaliyo katika Kumbukumbu la Torati sura ya 30.

Je, ni vigumu kujua na kufanya mambo ambayo Mungu anataka tufanye? * Musa anasema hivi: “Amri hii ninayokuamuru leo si ngumu mno kwako, wala haiko mbali.” (Mstari wa 11) Yehova hatuombi tufanye mambo ambayo hatuwezi kufanya. Matakwa yake ni yenye usawaziko na tunaweza kuyatimiza. Pia, tunaweza kuyajua. Si lazima tupande “mbinguni” au kusafiri kwenda “upande mwingine wa bahari” ili kujifunza mambo ambayo Mungu anataka tufanye. (Mstari wa 12, 13) Biblia inatuambia waziwazi jinsi ambavyo tunapaswa kuishi.—Mika 6:8.

Hata hivyo, Yehova hatulazimishi kumtii. Musa alisema hivi: “Naweka mbele yako leo uzima na mema, na kifo na mabaya.” (Mstari wa 15) Tuna uhuru wa kuchagua kati ya uzima na kifo, mema na mabaya. Tunaweza kuchagua kumwabudu na kumtii Mungu na kutazamia kupata baraka, au tunaweza kuchagua kutomtii na kupata matokeo mabaya. Ni juu yetu kuchagua tunalotaka.—Mstari wa 16-18; Wagalatia 6:7, 8.

Je, Yehova anachunguza kwa makini uamuzi tunaofanya? Bila shaka anachunguza! Musa aliongozwa na Mungu kusema hivi: ‘Chagueni uzima.’ (Mstari wa 19) Hata hivyo, tunaweza kuchagua uzima jinsi gani? Musa alieleza hivi: “Kwa kumpenda Yehova Mungu wako, kwa kuisikiliza sauti yake na kwa kushikamana naye.” (Mstari wa 20) Tukisitawisha upendo kwa Yehova, tutataka kumsikiliza kwa utii na kushikamana kabisa naye, katika hali yoyote ile. Tunapofanya hivyo, tunachagua uzima, yaani, tunachagua njia bora zaidi ya maisha sasa tukiwa na tumaini la kupata uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu unaokuja.—2 Petro 3:11-13; 1 Yohana 5:3.

Maneno ya Musa yanatufundisha kweli fulani inayotia nguvu imani yetu. Hata ikiwa umekabili hali gani katika ulimwengu huu mwovu, unaweza kufanikiwa; si lazima ushindwe. Yehova amekuheshimu kwa kukupa zawadi ya uhuru wa kuchagua. Ndiyo, unaweza kuchagua kumpenda Yehova, kumsikiliza, na kubaki mshikamanifu kwake. Ukichagua kufanya hivyo, Yehova atabariki jitihada zako.

Ukweli wa kwamba tuna uhuru wa kuchagua sisi wenyewe kumpenda na kumtumikia Yehova, ulimfariji mwanamke aliyetajwa mwanzoni mwa habari hii. Anasema hivi: “Ninampenda Yehova. Nyakati nyingine, ninasahau kwamba jambo la maana zaidi ni uhakika wa kwamba ninampenda Yehova. Kwa hiyo, ninaweza kuwa mwaminifu.” Kwa msaada wa Yehova, wewe pia unaweza kuwa mwaminifu.

[Maelezo ya chini]

^ fu. 2 Ona habari yenye kichwa “Mkaribie Mungu—Yehova Anataka Nini Kutoka Kwetu?” katika toleo la Oktoba 1, 2009 (1/10/2009), la Mnara wa Mlinzi.