Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kinachotuthibitishia Kweli Mungu Anatujali

Kinachotuthibitishia Kweli Mungu Anatujali

Kinachotuthibitishia Kweli Mungu Anatujali

KWA miaka mingi, watu wamejiuliza swali hili muhimu: Ikiwa Mungu anatupenda, kwa nini watu wanateseka sana? Huenda ukakubali kwamba ikiwa unampenda mtu, hungetaka kumwona akiteseka, na kama mtu huyo angepatwa na taabu yoyote, ungejaribu kumsaidia. Kwa kuwa kuna kuteseka kwingi ulimwenguni, watu wengi wanahisi kwamba Mungu hatujali. Kwa hiyo, ni muhimu kwanza tuzungumzie uthibitisho wa kwamba kweli Mungu anatupenda, kwamba Mungu anatujali.

Uumbaji Unathibitisha Upendo wa Mungu

Yehova Mungu ‘Ndiye aliyefanya mbingu na dunia na bahari na vitu vyote vilivyomo.’ (Matendo 4:24) Tunapotafakari vitu ambavyo Yehova amefanya, tunakata kauli kwamba anatujali. Kwa mfano, fikiria mambo yanayokufurahisha. Je, unapenda kula chakula kizuri? Ikiwa angetaka, Yehova angetupatia aina moja tu ya chakula ili kutegemeza uhai wetu. Lakini aliumba vyakula vya aina mbalimbali ili kufurahisha ulimi wetu. Vivyo hivyo, Yehova ameipamba dunia kwa miti, maua, na mandhari mbalimbali maridadi ili maisha yetu yafurahishe na kupendeza.

Pia, fikiria jinsi ambavyo tumeumbwa. Tunafurahia ucheshi, muziki, na tunathamini vitu maridadi. Uwezo huo wote si muhimu ili tuendelee kuishi lakini ni zawadi kutoka kwa Mungu ili kuboresha maisha yetu. Fikiria pia uhusiano wako na wengine. Kila mtu hufurahia kuwa pamoja na marafiki wazuri au kukumbatiwa na mtu anayempenda sana. Uwezo wa kupenda pia ni zawadi kutoka kwa Mungu mwenye upendo! Kwa kuwa Mungu aliwaumba wanadamu wakiwa na uwezo wa kuonyesha upendo, lazima sifa hiyo iwe sehemu ya utu wake.

Biblia Inatuthibitishia Upendo wa Mungu

Biblia inatuambia kwamba Mungu ni upendo. (1 Yohana 4:8) Upendo wake hauonekani tu katika uumbaji, bali pia katika Neno lake, Biblia. Kwa mfano, Biblia inatupa mwongozo wa jinsi ya kuwa na afya nzuri, inatutia moyo tuwe na kiasi katika mambo yote, na inatuonya kuhusu ulevi na ulafi.—1 Wakorintho 6:9, 10.

Biblia pia ina mashauri yenye hekima kuhusu jinsi ya kuwa na uhusiano mzuri na wengine, inatuhimiza tupendane na kuwatendea wengine kwa heshima na fadhili. (Mathayo 7:12) Inashutumu mazoea na mitazamo ambayo huwafanya watu wateseke—pupa, porojo, wivu, uzinzi, na uuaji. Ikiwa kila mtu angejitahidi kufuata mashauri mazuri yanayopatikana katika Maandiko, basi watu hawangeteseka sana ulimwenguni.

Hata hivyo, wonyesho mkubwa zaidi wa upendo wa Mungu ulikuwa kumtoa Mwana wake, Yesu, kuwa fidia kwa ajili ya wanadamu. Andiko la Yohana 3:16 linasema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.” Kwa sababu hiyo, tayari Yehova ameandaa njia ya kuondoa kifo na kuteseka kote.—1 Yohana 3:8.

Ni wazi kwamba kuna uthibitisho wa kutosha unaoonyesha kwamba Yehova anatupenda. Kwa hiyo, ni wazi kwamba Mungu hapendi kutuona tukiteseka. Atachukua hatua kukomesha kuteseka. Hatuhitaji kukisia-kisia kuhusu jambo hilo—Biblia inatueleza kwa njia hususa jinsi ambavyo Mungu atakomesha kuteseka.

[Picha katika ukurasa wa 4]

Uwezo wa kupenda ni zawadi kutoka kwa Mungu mwenye upendo