Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Alimmwagia Mungu Mahangaiko Yake Kupitia Sala

Alimmwagia Mungu Mahangaiko Yake Kupitia Sala

Igeni Imani Yao

Alimmwagia Mungu Mahangaiko Yake Kupitia Sala

HANA alikuwa akijitayarisha kwa ajili ya safari, huku akijaribu kusahau matatizo yake. Hiyo ilipaswa kuwa pindi yenye furaha; kila mwaka, Elkana, mume wake alikuwa na desturi ya kusafiri na familia yake yote kuelekea kwenye maskani huko Shilo. Yehova alitaka pindi hizo ziwe zenye shangwe. (Kumbukumbu la Torati 16:15) Na bila shaka tangu utotoni Hana alikuwa amefurahia sherehe hizo. Lakini mambo yalikuwa yamebadilika katika miaka ya hivi karibuni.

Hana alibarikiwa kuwa na mume anayempenda. Hata hivyo, Elkana alikuwa na mke mwingine. Aliitwa Penina, naye alikuwa ameazimia kufanya maisha ya Hana yawe yenye kujaa dhiki. Penina alitumia pindi hizo za kila mwaka kama mbinu ya kumfadhaisha sana Hana. Jinsi gani? Na jambo la muhimu hata zaidi, imani ya Hana katika Yehova ilimsaidia namna gani kukabiliana na hali hiyo iliyoonekana kuwa ngumu sana? Ukikabili matatizo yanayofanya usiwe na shangwe maishani, huenda kisa cha Hana kikakugusa moyo.

“Kwa Nini Moyo Wako Unahisi Vibaya?”

Biblia inaeleza matatizo mawili yaliyomkumba Hana. Angeweza kudhibiti kwa kiasi kidogo tatizo la kwanza, lakini hangeweza hata kidogo kudhibiti tatizo la pili. Kwanza, alikuwa katika ndoa ya wake wengi na mke mwenzake alimchukia. Pili, Hana alikuwa tasa. Hilo ni jambo gumu kwa mke yeyote anayetaka kuwa na watoto; lakini kulingana na tamaduni za siku za Hana jambo hilo lilileta huzuni kubwa. Kila familia ilitegemea watoto ili kuendeleza jina la familia. Kwa hiyo, kuwa tasa kulionwa kuwa suto na aibu.

Huenda Hana angekabiliana na hali yake ikiwa Penina hangemtaabisha. Ndoa ya wake wengi haikufaa hata kidogo. Mara nyingi ndoa hizo zilikuwa na mashindano, chuki, na uchungu. Hazikupatana na mpango wa ndoa ya mke moja ambayo Mungu alikuwa ameanzisha katika bustani ya Edeni. * (Mwanzo 2:24) Hali katika familia ya Elkana inaonyesha wazi kwamba Biblia haiungi mkono ndoa ya wake wengi.

Elkana alimpenda sana Hana. Hadithi za Kiyahudi zinasema kwamba alimwoa Hana kwanza na Penina aliolewa miaka kadhaa baadaye. Vyovyote vile, Penina alimwonea wivu Hana kwelikweli, na alitafuta njia za kumtaabisha mke mwenzake. Penina alijiona kuwa bora kwa sababu angeweza kuzaa. Alizaa mtoto mmoja baada ya mwingine, na kadiri watoto wake walivyoongezeka ndivyo kiburi chake kilivyoongezeka. Badala ya kumhurumia Hana na kumfariji, Penina alitumia hali yake ya kuwa tasa kumkera. Biblia inasema kwamba Penina alimsumbua mno Hana kiasi cha “kumfadhaisha.” (1 Samweli 1:6) Penina alifanya hivyo kimakusudi. Alitaka kumwumiza Hana, na alifaulu.

Inaonekana kwamba Penina alipata nafasi ya kumdhihaki Hana walipofunga safari za kila mwaka kwenda Shilo. Elkana alimpa kila mtoto wa Penina—“wanawe na binti zake wote”—fungu la dhabihu zilizotolewa kwa Yehova. Lakini Hana ambaye hakuwa na mtoto alipewa fungu moja tu. Penina alijitutumua sana kwa Hana na kumkumbusha kuhusu hali yake ya kuwa tasa hivi kwamba mwanamke huyo alilia sana na kukosa hamu ya kula. Elkana aliona kwamba mke wake mpendwa Hana alikuwa amefadhaika na hakuwa akila, hivyo alijaribu kumfariji. Alimwuliza: “Hana, kwa nini unalia, na kwa nini huli chakula, na kwa nini moyo wako unahisi vibaya? Je, mimi si bora kwako kuliko wana kumi?”—1 Samweli 1:4-8.

Elkana alitambua kwamba Hana alifadhaika kwa sababu alikuwa tasa. Na Hana alithamini sana jinsi Elkana alivyompenda kwa wororo. * Elkana hakutaja kuhusu chuki ya Penina, wala Biblia haisemi kwamba Hana alimwambia jambo hilo. Labda alihisi kwamba kumshitaki Penina kungefanya hali yake iwe mbaya hata zaidi. Je, Elkana angebadili hali hiyo? Je, hilo halingemfanya Penina amchukie Hana hata zaidi na kuwafanya watoto na watumishi wamwige Penina? Hilo lilifanya Hana ahisi kuwa ametengwa kabisa katika nyumba yake mwenyewe.

Iwe Elkana alijua yale ambayo Penina alikuwa akimtendea Hana au la, Yehova aliyaona yote yaliyokuwa yakitendeka. Neno lake linafunua mambo yote hayo, na hivyo kutoa onyo kwa wote walio na tabia ya kuwaonea wengine wivu na kuwachukia. Kwa upande mwingine, watu wasio na hatia na wenye kufanya amani kama Hana wanaweza kufarijika kujua kwamba Mungu wa haki atasuluhisha mambo kwa njia yake na kwa wakati wake. (Kumbukumbu la Torati 32:4) Huenda Hana alijua jambo hilo kwa kuwa alimwomba Yehova msaada.

‘Hakuonyesha Tena Kuhangaika’

Asubuhi na mapema, familia nzima ilikuwa na pilikapilika nyingi. Kila mtu alikuwa akijitayarisha kwa ajili ya safari, kutia ndani watoto. Safari hiyo ya kwenda Shilo ilikuwa ya kilomita 30 kuvuka nchi ya Efraimu yenye milima-milima. * Safari hiyo ingechukua siku moja au mbili kwa miguu. Hana alijua jinsi mke mwenzake angemtendea. Hata hivyo, Hana hakubaki nyumbani. Hivyo anawawekea waabudu wa Mungu leo mfano mzuri. Si jambo la hekima kuruhusu mwenendo wa wengine utuzuie tusimwabudu Mungu. Ikiwa tutafanya hivyo tutakosa baraka zitakazotuwezesha kuvumilia.

Baada ya safari ndefu ya siku moja kupitia milima iliyokuwa na barabara zilizojipinda-pinda, familia hiyo kubwa ilikaribia Shilo. Jiji hilo lilikuwa juu ya mlima likiwa limezungukwa na milima mingine mirefu. Walipokuwa wakilikaribia, huenda Hana alitafakari yale ambayo angemwambia Yehova katika sala. Mara tu walipofika familia hiyo ilikula pamoja. Hana alipopata nafasi, mara moja aliondoka na kwenda kwenye maskani ya Yehova. Kuhani Mkuu Eli alikuwa ameketi karibu na mwimo wa mlango wa hekalu. Lakini Hana alikazia fikira Mungu wake. Alikuwa na uhakika kwamba angesikiwa akiwa katika maskani. Hata kama hakuna mwanadamu ambaye angeweza kuelewa hali yake yenye kufadhaisha, Baba yake aliye mbinguni angemwelewa. Uchungu ulimjaa moyoni hivi kwamba akaanza kulia.

Huku mwili wake ukitetemeka kwa sababu ya kulia, Hana alimweleza Yehova shida zake kimoyomoyo. Midomo yake ilitetemeka akitafuta maneno ya kueleza uchungu wake. Alisali kwa muda mrefu, akimmwagia Baba yake yaliyokuwa moyoni mwake. Hata hivyo, alifanya mengi zaidi ya kumwomba Mungu atimize tamaa yake ya kupata mtoto. Hana hakutamani tu kupata baraka za Mungu bali pia alitaka kumpa Mungu chochote ambacho angeweza. Kwa hiyo, aliweka nadhiri akisema kwamba ikiwa angepata mtoto wa kiume angemtoa ili amtumikie Yehova.—1 Samweli 1:9-11.

Hivyo, Hana anawawekea watumishi wote wa Yehova mfano mzuri kuhusu sala. Yehova anawaalika watumishi wake wawasiliane naye kwa uhuru, bila kusitasita, wakimmiminia mahangaiko yao kama vile tu ambavyo mtoto anayemwamini baba yake mwenye upendo hufanya. (Zaburi 62:8; 1 Wathesalonike 5:17) Mtume Petro aliongozwa na roho kuandika maneno haya yenye kufariji kuhusu kusali kwa Yehova: ‘Tupeni mahangaiko yenu yote juu yake, kwa sababu yeye anawajali ninyi.’—1 Petro 5:7.

Hata hivyo, tofauti na Yehova, wanadamu hawaelewi wala hawana huruma. Hana alipokuwa akilia na kusali alishtuka kusikia sauti ya mtu fulani. Ilikuwa sauti ya Eli, kuhani mkuu, ambaye alikuwa amemtazama. Eli alimwambia hivi: “Utaendelea kujiendesha kama mlevi mpaka wakati gani? Iondolee mbali divai yako.” Eli aliona midomo ya Hana ikitetemeka, huku akilia, na akiwa na huzuni nyingi. Badala ya kumwuliza tatizo lake, Eli alikata kauli haraka kwamba Hana alikuwa mlevi.—1 Samweli 1:12-14.

Kushutumiwa bila msingi wowote, hasa na mwanamume aliye na cheo chenye kuheshimika kulimwumiza Hana sana, hasa wakati huu alipokuwa amefadhaika sana. Hata hivyo, aliweka tena mfano mzuri wa imani. Hakuruhusu kutokamilika kwa mwanadamu kumzuie kumwabudu Yehova. Alimjibu Eli kwa heshima na akamweleza hali yake. Eli alipotambua kuwa amekosea, alimjibu hivi kwa upole: “Nenda kwa amani, naye Mungu wa Israeli akupe ombi lako ambalo umemwomba.”—1 Samweli 1:15-17.

Hana alipommiminia Yehova moyo wake na kumwabudu katika maskani, kulikuwa na matokeo gani? Simulizi hilo linasema: “Mwanamke huyo akaenda zake, akala chakula, na uso wake haukuonyesha tena kuhangaika.” (1 Samweli 1:18) Biblia Habari Njema inasema: “Hakuwa na huzuni tena.” Hana alihisi ametulia. Ni kana kwamba alikuwa amechukua mzigo wake wa hisia zilizokuwa zikimfadhaisha na kumtupia Yehova, Baba yake wa mbinguni mwenye nguvu. (Zaburi 55:22) Je, Yehova anaweza kushindwa na tatizo lolote? La—hakuna lolote lililomshinda jana, linaloweza kumshinda leo, wala kesho!

Tunapohisi tumelemewa na hisia au kuhuzunika kupita kiasi, tunaweza kumwiga Hana na kuzungumza waziwazi na Yule ambaye Biblia inamwita “msikiaji wa sala.” (Zaburi 65:2) Tukisali kwa imani, huenda tukaacha kuhuzunika na badala yake tukawa na “amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote.”—Wafilipi 4:6, 7.

“Hakuna Mwamba Ulio Kama Mungu Wetu”

Asubuhi iliyofuata, Hana alirudi kwenye maskani akiwa na Elkana. Huenda alimweleza kuhusu ombi lake na nadhiri aliyoweka, kwa kuwa Sheria ya Musa ilisema kwamba mume alikuwa na haki ya kufutilia mbali nadhiri iliyowekwa na mke wake bila ruhusa yake. (Hesabu 30:10-15) Lakini mwanamume huyo mwaminifu hakufanya hivyo. Badala yake, yeye na Hana walimwabudu Yehova kwenye maskani kisha wakarudi nyumbani.

Ni wakati gani ambapo Penina alitambua kuwa hangeweza tena kumhuzunisha Hana? Simulizi halitaji hilo, lakini maneno uso wa Hana “haukuonyesha tena kuhangaika” yanaonyesha kwamba kuanzia wakati huo Hana alidumisha furaha yake. Kwa vyovyote vile, Penina aligundua kwamba hata afanye jambo gani lenye kuudhi, Hana hakuhangaishwa na mambo hayo. Biblia haimtaji Penina tena.

Kadiri miezi ilivyopita, amani ya akili ambayo Hana alikuwa nayo iliongezeka na kuwa furaha nyingi. Alikuwa mja-mzito! Shangwe yake haikumfanya asahau ni nani aliyekuwa amembariki. Mvulana wake alipozaliwa, alimpa jina Samweli, linalomaanisha “Jina la Mungu” na kwa wazi linarejelea kuliitia jina la Mungu, kama Hana alivyokuwa amefanya. Mwaka huo, hakuandamana na Elkana na familia yake kwenda Shilo. Alikaa nyumbani na mtoto huyo kwa miaka mitatu, hadi alipomwachisha kunyonya. Kisha akajitayarisha kwa ajili ya siku ambayo angetengana na mwana wake mpendwa.

Ni wazi kwamba haingekuwa rahisi kutengana na mwana wake. Bila shaka, Hana alijua kwamba Samweli angetunzwa vizuri huko Shilo, labda angetunzwa na wanawake fulani waliotumikia kwenye maskani. Lakini, bado alikuwa mchanga, na ni mama gani ambaye hatamani kuwa pamoja na mtoto wake? Hata hivyo, Hana na Elkana walimpeleka mvulana huyo, si kwa kulazimishwa bali kwa kupenda. Walitoa dhabihu katika nyumba ya Mungu, wakamkabidhi Samweli kwa Eli, na kumkumbusha kuhusu nadhiri ambayo Hana alikuwa ameweka miaka kadhaa iliyopita.

Kisha Hana akatoa sala ambayo Mungu aliona inastahili kutiwa katika Neno lake lililoongozwa na roho. Unaposoma maneno yake yaliyoandikwa katika 1 Samweli 2:1-10, utaona kwamba kila mstari unaonyesha kwamba alikuwa na imani yenye nguvu. Alimsifu Yehova kwa kutumia nguvu zake kwa njia ya ajabu—kwa uwezo wake usio na kifani wa kuwashusha wenye majivuno, kuwabariki walioonewa, na wa kuua au kuhifadhi uhai. Alimsifu Baba yake kwa utakatifu wake wa pekee, haki yake, na uaminifu wake. Hana angeweza kusema hivi akiwa na sababu nzuri: “Hakuna mwamba ulio kama Mungu wetu.” Yehova anategemeka kabisa, habadiliki, na ni kimbilio kwa ajili ya wote walioonewa na kukandamizwa na ambao wanamwomba msaada.

Kijana Samweli alikuwa na pendeleo kubwa la kuwa na mama aliyekuwa na imani nyingi katika Yehova. Ingawa alimkosa sana mama yake alipokuwa akikua, hakuhisi amesahaulika. Mwaka baada ya mwaka, Hana angerudi Shilo, akiwa na koti dogo lisilo na mikono ambalo Samweli angevaa alipokuwa akimtumikia Yehova katika maskani. Kumshonea koti hilo kulionyesha wazi kwamba anampenda na kumjali mwana wake. (1 Samweli 2:19) Tunaweza kuwazia akimvisha mvulana wake koti hilo, akilinyoosha, na kumtazama kwa upendo huku akizungumza naye kwa fadhili na kwa njia yenye kutia moyo. Samweli alibarikiwa sana kuwa na mama kama huyo, naye akaja kuwa baraka kubwa kwa wazazi wake na kwa Israeli yote.

Hana naye hakusahauliwa. Yehova alimbariki kwa kumrudishia uwezo wa kuzaa, naye akamzalia Elkana watoto wengine watano. (1 Samweli 2:21) Hata hivyo, huenda baraka kubwa zaidi ambayo Hana alipata ilikuwa kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Baba yake, Yehova, ambao uliendelea kuimarika kadiri ambavyo miaka ilipita. Wewe pia na upate baraka hiyo, unapoiga imani ya Hana.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 7 Ili ujue ni kwa nini Mungu aliruhusu ndoa ya wake wengi kati ya watu wake kwa muda fulani, ona habari yenye kichwa “Je, Mungu Anakubali Ndoa ya Wake Wengi?” ukurasa wa 30 katika Mnara wa Mlinzi la Julai 1, 2009 (1/7/2009).

^ fu. 10 Ingawa Biblia inasema kwamba Yehova alikuwa ‘amefunga tumbo la uzazi la Hana,’ hilo halithibitishi kuwa Yehova hakupendezwa na mwanamke huyo mwaminifu na mnyenyekevu. (1 Samweli 1:5) Nyakati nyingine Biblia husema kuwa Mungu amefanya mambo fulani kwa kuwa tu ameyaruhusu yatendeke kwa muda fulani.

^ fu. 13 Huenda umbali huo ulikadiriwa hivyo kwa sababu mji wa Rama ambako Elkana aliishi ni mji uliokuja kuitwa Arimathea katika siku za Yesu.

[Sanduku katika ukurasa wa 17]

Sala Mbili za Pekee

Sala mbili za Hana zilizoandikwa katika 1 Samweli 1:11 na 2:1-10, zina mambo mengi yenye kupendeza. Fikiria mifano ifuatayo:

▪ Hana alielekeza sala yake ya kwanza kwa “Yehova wa majeshi.” Yeye ndiye mtu wa kwanza katika Biblia anayenukuliwa kuwa alitumia jina hilo la cheo. Jina hilo linapatikana mara 285 katika Biblia na linarejelea uwezo ambao Mungu anao juu ya jeshi kubwa la wana wa roho.

▪ Ona kwamba Hana alitoa sala ya pili, si wakati mwana wake alipozaliwa, bali wakati yeye na Elkana walipomtoa kwa ajili ya utumishi wa Mungu huko Shilo. Kwa hiyo, shangwe ya Hana haikutokana na kumnyamazisha mke mwenzake, Penina, lakini ilitokana na baraka za Yehova.

▪ Hana aliposema, “Pembe yangu kweli imeinuliwa katika Yehova,” huenda akilini alikuwa akimfikiria ng’ombe-dume, mnyama ambaye hutumia pembe zake kwa nguvu. Ni kana kwamba Hana alikuwa akisema: ‘Yehova, wewe ndiye unayenitia nguvu.’—1 Samweli 2:1.

▪ Maneno ya Hana kuhusu “mtiwa-mafuta” wa Mungu ni ya kinabii. Neno hilo ni sawa na “masihi,” naye Hana ndiye mtu wa kwanza katika Biblia kurejelea mfalme mtiwa-mafuta wa wakati ujao.—1 Samweli 2:10.

▪ Miaka 1,000 hivi baadaye, Maria, mama ya Yesu, alitumia maneno fulani ya Hana alipokuwa akimsifu Yehova.—Luka 1:46-55.

[Picha katika ukurasa wa 16]

Hana alihuzunishwa sana kwa sababu alikuwa tasa, na Penina alifanya kila kitu kumwudhi

[Picha katika ukurasa wa 16, 17]

Je, unaweza kuiga mfano wa Hana wa kusali kutoka moyoni?

[Picha katika ukurasa wa 17]

Ingawa Eli alimshutumu bila msingi, Hana hakumkasirikia