Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Kwa nini watu katika nyakati za Biblia walitumia lami kama saruji?

Biblia inapozungumza kuhusu wajenzi wa mnara wa Babeli, inasema kwamba ‘matofali yalikuwa mawe yao, lakini lami ilikuwa saruji yao.’​—Mwanzo 11:3.

Lami ni mali ya asili. Inatokana na mafuta, nayo hupatikana kwa wingi huko Mesopotamia, ambako hububujika kutoka ardhini na kisha kuganda. Uwezo wake wa kunata ulijulikana katika nyakati za Biblia. Lami “ilifaa sana kwa ujenzi wa nyumba zilizotengenezwa kwa matofali yaliyochomwa,” kinasema kitabu kimoja cha marejeo.

Makala moja katika gazeti Archaeology inaeleza kuhusu matembezi ya hivi karibuni kwenye mabaki ya mnara katika jiji la kale la Uru, huko Mesopotamia. “Saruji ya lami​—mojawapo ya matumizi ya kwanza ya lami katika eneo kubwa la kusini mwa Iraki lenye mafuta​—​bado inaonekana katikati ya matofali yaliyochomeka,” anasema mwandishi. “Lami hiyo nyeusi yenye kunata, ambayo leo ni chanzo cha msukosuko na jeuri katika eneo hilo, wakati fulani iliunganisha ustaarabu wa eneo hilo. Kutumia lami kama saruji na katika kutengeneza vijia kumesaidia matofali ya udongo ya Sumeria yasiharibiwe na maji na hivyo kuhakikisha kwamba kuta zilidumu kwa muda mrefu sana.”

Ni “karatasi” za aina gani ambazo zilitumiwa katika nyakati za Biblia?

Swali hilo huwa linazuka kwa sababu ya maneno ya mwandishi wa Biblia Yohana: “Ijapokuwa nina mambo mengi ya kuwaandikia ninyi, sitaki kufanya hivyo kwa karatasi na wino.”​—2 Yohana 12.

Neno la Kigiriki kharʹtes hapa linalotafsiriwa kuwa “karatasi,” linarejelea karatasi zilizotengenezwa kwa mafunjo, mimea inayokua ndani ya maji. Kitabu kimoja cha marejeo kinaeleza hivi kuhusu mbinu iliyotumiwa kutengeneza karatasi hizo za kuandikia kutoka kwa shina la mimea: “Mashina, ambayo labda yalikuwa na urefu wa mita tatu, yaliambuliwa maganda na kukatwa katika vipande virefu ambavyo viliunganishwa pamoja na kuwa matabaka, nyuzi-nyuzi katika matabaka hayo zilipangwa kutoka juu kwenda chini na kutoka kushoto kwenda kulia, kisha karatasi hizo zilipigwa-pigwa kwa nyundo ya mbao na mwishowe kulainishwa kwa chombo cha kuparuza.”

Wataalamu wa vitu vya kale wamepata hati nyingi za kale zilizoandikwa kwenye mafunjo huko Misri na maeneo yaliyo karibu na Bahari ya Chumvi. Mafunjo fulani ya Kimaandiko yaliyopatikana katika maeneo hayo yaliandikwa kipindi cha Yesu au hata kabla ya hapo. Inawezekana kwamba karatasi hizo ndizo zilizotumiwa kuandika barua zilizo katika Biblia, kama vile barua zilizoandikwa na mitume.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 11]

Spectrumphotofile/ photographersdirect.com

© FLPA/​David Hosking/​age fotostock