Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wakristo walikimbia kutoka Yudea kabla ya uharibifu wa Yerusalemu mwaka wa 70 W.K.?

“Mtakapoona Yerusalemu limezingirwa na majeshi yaliyopiga kambi, ndipo jueni kwamba kufanywa ukiwa kwake kumekaribia. Ndipo wale walio katika Yudea waanze kukimbilia milimani, na wale walio katikati yake na waondoke.” (Luka 21:20, 21) Yesu aliwapa wanafunzi wake maagizo hayo yaliyohusu uharibifu ambao ungekuja juu ya Yerusalemu. Je, kuna uthibitisho wowote kwamba wanafunzi walitii onyo la Yesu?

Miongo kadhaa baada ya kifo cha Yesu, Sesho Galo aliamuru jeshi la Roma liingie Palestina ili kukomesha uasi wa Wayahudi. Uvamizi huo ulithibitishwa na mwanahistoria Myahudi Yosefo, ambaye aliishi wakati huo. Wanajeshi Waroma walizingira Yerusalemu na inaonekana kwamba walikuwa na uhakika wa kulishinda jiji hilo. Kwa ghafla, Galo akaamuru wanajeshi wake waondoke. Kulingana na Eusebio, mwanahistoria wa mambo ya kanisa, Wakristo walioishi Yudea walitumia fursa hiyo kukimbilia Pela, jiji lililokuwa kwenye eneo lenye milima ya Dekapoli.

Miaka kadhaa baadaye, katika mwaka wa 70 W.K., jeshi lingine la Roma likiongozwa na Jenerali Tito lilirudi na kuzingira jiji kuu la Wayahudi. Wakati huu wanajeshi waliliharibu jiji hilo, jambo ambalo wanajeshi wa Galo hawakufanya. Mamia ya maelfu ya watu walinaswa jijini Yerusalemu na wakafa.

“Wana wa manabii” walikuwa nani?

Masimulizi ya Biblia kuhusu nabii Samweli, Eliya, na Elisha hurejelea wanaume walioitwa “wana wa manabii.” Kwa mfano, Elisha alimtuma “mmoja wa wana wa manabii” ili amtie mafuta Yehu awe mfalme wa Israeli.—2 Wafalme 9:1-4.

Wasomi fulani huamini kwamba maneno “wana wa manabii” hayamaanishi uzao wa manabii bali hurejelea kikundi cha watu walioishi na kufanya kazi pamoja. Kulingana na gazeti Journal of Biblical Literature, huenda washiriki wa vikundi hivyo walikuwa watu waliokuwa “wamejitoa wenyewe katika utumishi wa Yahweh [Yehova] chini ya nabii aliyekuwa . . . baba yao wa kiroho.” (2 Wafalme 2:12) Simulizi la kutiwa mafuta kwa Yehu, linamtaja mjumbe wa Elisha kama “mtumishi wa nabii.”—2 Wafalme 9:4.

Inaonekana kwamba “wana wa manabii” waliishi maisha rahisi. Inasemekana kwamba kikundi kimoja katika nyakati za Elisha walijijengea mahali pa kuishi na walitumia shoka la kuazimwa. (2 Wafalme 6:1-5) Baadhi ya watu katika makundi hayo walikuwa wameoa na jambo hilo linaonyeshwa kwa kuwepo kwa wajane wa “wana wa manabii.” (2 Wafalme 4:1) Ni wazi kwamba Waisraeli waaminifu waliwathamini wana wa manabii, na simulizi moja linataja kwamba waliwapa zawadi za vyakula.​—2 Wafalme 4:38, 42.