Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU | JE, MUNGU ANAKUJALI?

Mungu Anakuelewa

Mungu Anakuelewa

“Ee Yehova, umenichunguza kabisa, nawe unanijua.”—ZABURI 139:1.

“Macho yako yalikiona kiini-tete changu.” —ZABURI 139:16

KWA NINI WENGINE HAWAAMINI? Watu wengi wanahisi kwamba Mungu huwaona wanadamu kuwa wenye dhambi—wasio safi na wasiofaa. Kendra, aliyepatwa na ugonjwa wa kushuka moyo, alijihisi mwenye hatia sana kwa sababu alidhani hangeweza kufuata viwango vya Mungu kikamili. Kwa hiyo, anasema: “Niliacha kusali.”

BIBLIA INAFUNDISHA NINI? Yehova haangalii tu dhambi zako bali pia anaelewa vizuri kabisa utu wako. Biblia inasema: “Analijua vema umbo letu. Akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.” Zaidi ya hayo, hashughuliki nasi “kulingana na makosa yetu” bali anatusamehe kwa rehema tunapotubu.—Zaburi 103:10, 14.

Mfikirie Daudi, mfalme wa Israeli aliyetajwa kwenye makala ya kwanza ya mfululizo huu. Alipokuwa akisali kwa Mungu alisema hivi: “Macho yako yalikiona kiini-tete changu, na katika kitabu chako sehemu zake zote zilikuwa zimeandikwa . . . Unichunguze kabisa, Ee Mungu, uujue moyo wangu.” (Zaburi 139:16, 23) Naam, Daudi alikuwa na hakika kwamba ingawa alitenda dhambi—hata dhambi nzito—Yehova angeweza kutambua moyo wake wenye toba.

Yehova anakuelewa vizuri zaidi kuliko binadamu yeyote yule. Biblia inasema: “Mwanadamu huona kile kinachoonekana kwa macho, lakini Yehova huona jinsi moyo ulivyo.” (1 Samweli 16:7) Mungu anakujua kwa undani, yaani, chembe za urithi, malezi, mazingira, na mambo yote yanayochangia utu wako. Mungu anaona na kuthamini jitihada zako za kuwa mtu mwema, hata ingawa unakosea.

Hata hivyo, Mungu hutumiaje mambo anayojua kukuhusu ili kukusaidia?