Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAZUNGUMZO PAMOJA NA JIRANI

Ufalme wa Mungu Ulianza Kutawala Lini? (Sehemu ya 2)

Ufalme wa Mungu Ulianza Kutawala Lini? (Sehemu ya 2)

Mazungumzo yafuatayo yanaonyesha jinsi Shahidi wa Yehova anavyoweza kuzungumza na jirani yake. Hebu tuwazie Shahidi anayeitwa Cameron amemtembelea tena mwanamume anayeitwa Jon nyumbani kwake.

NDOTO YA NEBUKADNEZA—TAARIFA FUPI

Cameron: Ninafurahi kukuona tena Jon. Ninafurahia sana mazungumzo yetu ya Biblia ya kila juma. * Unaendeleaje?

Jon: Nashukuru, ninaendelea vizuri.

Cameron: Ninafurahi kusikia hivyo. Mara ya mwisho nilipokuwa hapa, tulizungumzia kwa nini Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba Ufalme wa Mungu ulianza kutawala mwaka wa 1914. * Kama tulivyozungumzia tunapata uthibitisho mkubwa katika unabii ulio kwenye sura ya 4 ya kitabu cha Biblia cha Danieli. Je, unakumbuka unabii huo?

Jon: Ndiyo, ulikuwa kuhusu ndoto ya Mfalme Nebukadneza ya mti mkubwa.

Cameron: Ndiyo, kweli kabisa. Katika ndoto hiyo, Nebukadneza aliona mti mrefu uliofika mbinguni. Vilevile, alimsikia mjumbe wa Mungu akiamuru kwamba mti huo ukatwe, lakini kisiki na mizizi yake iachwe kwenye udongo. Baada ya kipindi cha “nyakati saba,” mti huo ungekua tena. * Tulizungumzia pia jinsi unabii huo ulivyotimizwa kwa njia mbili. Je, unakumbuka utimizo wa kwanza?

Jon: Ulimhusu Nebukadneza mwenyewe, au sivyo? Alipatwa na wazimu kwa miaka saba.

Cameron: Sawa kabisa. Nebukadneza alipatwa na wazimu kwa muda, hivyo utawala wake ulikatizwa. Lakini, katika utimizo mkubwa zaidi wa unabii huo, utawala wa Mungu duniani ungekatizwa kwa kipindi cha nyakati saba. Kama tulivyoona, nyakati saba zilianza Yerusalemu lilipoharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. Kuanzia mwaka huo, hakukuwa tena na wafalme duniani waliomwakilisha Yehova Mungu katika kuwatawala watu wake. Hata hivyo, mwishoni mwa nyakati saba, Mungu angeweka mtawala ambaye angemwakilisha, hangekuwa duniani, bali mbinguni. Kwa maneno mengine, kukamilika kwa zile nyakati saba kungeonyesha kwamba Ufalme wa mbinguni wa Mungu umeanza kutawala. Kufikia sasa, tumeona zile nyakati saba zilianza lini. Hivyo ikiwa tunaweza kujua zilikuwa na urefu gani, tutajua wakati ambapo Ufalme wa Mungu ulianza kutawala. Je, tuko pamoja kufikia hapo?

Jon: Ndiyo, taarifa hizo zimenisaidia kukumbuka.

Cameron: Safi. Acha sasa tuanze mazungumzo yetu, na tuchunguze urefu wa hizo nyakati saba. Nilipitia habari hii ili nijikumbushe mambo makuu. Nitajitahidi kuyaeleza kadiri niwezavyo.

Jon: Sawa.

 NYAKATI SABA ZAISHA —SIKU ZA MWISHO ZAANZA

Cameron: Katika utimizo wa kwanza wa unabii huo uliomhusu Nebukadneza, nyakati saba zilikuwa miaka saba halisi. Lakini katika utimizo mkubwa zaidi uliohusu Ufalme wa Mungu, nyakati saba zilikuwa ndefu kuliko miaka saba halisi.

Jon: Kwa nini?

Cameron: Kwa sababu, kwanza, kumbuka nyakati saba zilianza Yerusalemu lilipoharibiwa mwaka wa 607 K.W.K. Tukihesabu miaka saba halisi kuanzia mwaka huo, tutafikia mwaka wa 600 K.W.K. Hata hivyo, hakuna jambo lolote muhimu linalohusiana na utawala wa Mungu lililotukia mwaka huo. Isitoshe, kama tulivyoona, Yesu alipokuwa duniani karne nyingi baadaye, alithibitisha kwamba nyakati saba hazikuwa zimeisha.

Jon: Aah, ndiyo. Sasa nakumbuka.

Cameron: Hivyo, nyakati saba si miaka saba halisi, bali zinawakilisha kipindi kirefu cha wakati.

Jon: Kipindi hicho kina urefu gani?

Cameron: Kitabu cha Biblia cha Ufunuo ambacho ujumbe wake unakaribiana sana na ule wa kitabu cha Danieli, kinatusaidia kujua urefu wa zile nyakati saba. Kinaonyesha kwamba kipindi cha nyakati tatu na nusu kina urefu wa siku 1,260. * Hivyo, nyakati saba—ambazo ni mara mbili ya nyakati tatu na nusu—zina urefu wa siku 2,520. Je, bado tuko pamoja?

Jon: Ndiyo, ninakuelewa. Hata hivyo, sioni jinsi hilo linavyoonyesha kwamba Ufalme wa Mungu ulianza kutawala mwaka wa 1914.

Cameron: Sawa, acha tuone kama tunaweza kuelewa jinsi habari hizo zinavyohusiana. Nyakati nyingine katika unabii wa Biblia, siku moja huwakilisha mwaka mmoja. * Tukitumia kanuni ya siku moja kwa mwaka mmoja, nyakati hizo saba zitakuwa na urefu wa miaka 2,520. Tukihesabu miaka 2,520 kuanzia 607 K.W.K., tunafikia mwaka wa 1914. * Hivyo ndivyo tunavyopata jibu kwamba 1914 ndio mwaka ambao zile nyakati saba zilikamilika, na Yesu akaanza kutawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Isitoshe, tangu mwaka wa 1914, kumekuwa na matukio makubwa ulimwenguni—matukio ambayo Biblia ilitabiri kuhusiana na siku za mwisho.

Jon: Matukio gani?

Cameron: Fikiria yale aliyosema Yesu kwenye Mathayo 24:7. Akizungumza kuhusu wakati ambapo angeanza kutawala mbinguni, Yesu alisema hivi: “Taifa litasimama kupigana na taifa na ufalme kupigana na ufalme, kutakuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya nchi mahali pamoja baada ya pengine.” Ona kwamba Yesu alitabiri kungekuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya nchi katika kipindi hicho. Dunia yetu imepata matatizo mengi kama hayo katika karne iliyopita, sivyo?

Jon: Ndiyo.

Cameron: Katika mstari huo, Yesu alitabiri pia kungekuwa na vita anapotawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu. Na kitabu cha Biblia cha Ufunuo kilitabiri kwamba kungekuwa na vita ambavyo vingewaathiri watu duniani kote wakati huo wa mwisho. * Je, unakumbuka vita vya ulimwengu vya kwanza vilitokea lini?

Jon: Vilitokea mwaka wa 1914, mwaka uleule  ambao ulisema Yesu alianza kutawala! Sikujua mambo hayo yana uhusiano.

Cameron: Tunapounganisha habari hizo pamoja, yaani, unabii kuhusu zile nyakati saba na unabii mwingine unaohusu siku za mwisho, ni sahihi kabisa. Mashahidi wa Yehova wanaamini kwamba Yesu alianza kutawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu mwaka wa 1914, na kwamba siku za mwisho zilianza mwaka huo. *

Jon: Bado ninajitahidi kuyaelewa kabisa hayo yote.

Cameron: Hakuna tatizo. Kama nilivyokueleza, mimi pia sikuelewa mara moja. Lakini angalau, natumaini umeona kwamba hata ingawa mwaka wa 1914 hautajwi kihususa katika Biblia, yale ambayo Mashahidi wa Yehova waamini kuhusu mwaka huo yanategemea Maandiko.

Jon: Ndiyo, ninapenda jinsi mnavyotumia Maandiko kuthibitisha jambo lolote mnalosema. Hamsemi maoni yenu. Hata hivyo, bado najiuliza, kwa nini habari hiyo si rahisi kuelewa? Kwa nini Mungu hakusema tu moja kwa moja katika Biblia kwamba Yesu angeanza kutawala mbinguni mwaka wa 1914?

Cameron: Jon, hilo ni swali zuri. Kwa kweli, kuna mambo mengi ambayo hayajafafanuliwa moja kwa moja katika Maandiko. Kwa nini Mungu alielekeza Biblia iandikwe kwa njia ambayo watu wangehitaji jitihada ili waelewe? Labda tunaweza kuzungumzia hilo nitakaporudi.

Jon: Nitafurahi, karibu tena.

Je, kuna jambo lolote kuhusu Biblia ambalo limekuwa likikutatiza? Je, kuna jambo lolote ambalo Mashahidi wa Yehova wanaamini au kufanya ambalo ungependa kulifahamu zaidi? Ikiwa ndivyo, utakapokutana tena na Mashahidi wa Yehova usikose kuwauliza. Watafurahi kuzungumzia jambo hilo pamoja nawe.

^ fu. 5 Kupitia mpango wao wa kujifunza Biblia na watu nyumbani kwao bila malipo, Mashahidi wa Yehova hutumia utaratibu fulani ili kuwafundisha Biblia.

^ fu. 7 Ona makala “Mazungumzo Pamoja na Jirani—Ufalme wa Mungu Ulianza Kutawala Lini?—Sehemu ya 1” katika toleo la Oktoba 1, 2014 la gazeti hili.

^ fu. 24 Ona chati “Ndoto ya Nebukadneza ya Mti.”

^ fu. 30 Ona sura ya 9 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.