Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU | JE, KUNA FAIDA YOYOTE TUNAPOSALI?

Je, Kuna Yeyote Anayesikiliza Sala?

Je, Kuna Yeyote Anayesikiliza Sala?

Baadhi ya watu huona kwamba kutoa sala ni kupoteza muda kwa sababu hakuna anayesikiliza. Wengine wamesali lakini wanahisi kwamba sala zao hazijajibiwa. Mtu mmoja aliyeamini kwamba hakuna Mungu aliamua kusali hivi siku moja: “Tafadhali ongea nami hata kidogo.” Lakini alisema kwamba Mungu “alikaa kimya.”

Hata hivyo, Biblia inatuhakikishia kwamba Mungu husikiliza sala. Biblia inasema hivi tangu zamani: “Yeye [Mungu] hakika atakuonyesha kibali unapotoa sauti ya kilio chako; mara tu atakapokisikia kwa kweli atakujibu.” (Isaya 30:19) Mstari mwingine unaopatikana katika Biblia unasema hivi: “Sala ya wanyoofu ni furaha kwake.”—Methali 15:8.

Yesu alisali kwa Baba yake, “naye akasikiwa vizuri.”—Waebrania 5:7

Biblia inataja pia mifano ya watu ambao sala zao zilisikilizwa. Mstari mmoja unasema kwamba Yesu alitoa “maombi kwa Yule aliyekuwa na uwezo wa kumwokoa” na “akasikiwa vizuri.” (Waebrania 5:7) Mifano mingine inapatikana katika Danieli 9:21 na 2 Mambo ya Nyakati 7:1.

Hivyo, kwa nini watu fulani huhisi kwamba sala zao hazijibiwi? Ili sala zetu zisikilizwe, tunapaswa kusali kwa Yehova, * ambaye ni Mungu pekee anayetajwa katika Biblia, wala si kwa mungu mwingine au mababu. Mungu pia anataka ‘tuombe kulingana na mapenzi yake,’ yaani, mambo anayopenda. Mungu anatuhakikishia kwamba tukisali kwa njia hiyo, ‘yeye atatusikia.’ (1 Yohana 5:14) Hivyo, ili sala zetu zisikilizwe, tunahitaji kumjua Mungu anayetajwa katika Biblia na kujifunza kuhusu mapenzi yake.

Watu wengi wanaamini kwamba sala si jambo la kidini tu bali Mungu husikiliza na kujibu sala. Isaac, kutoka Kenya, anasema hivi: “Nilisali ili nipate msaada wa kuielewa Biblia. Muda mfupi baadaye, mtu fulani alikuja na kunisaidia kuielewa Biblia.” Hilda anayeishi nchini Ufilipino, alitaka kuacha kuvuta sigara. Baada ya kuona anashindwa, mume wake alimshauri hivi: “Kwa nini usimwombe Mungu akusaidie?” Alitii ushauri huo na anasema hivi: “Ninashangaa jinsi Mungu alivyonisaidia. Nilianza kupoteza hamu ya kuvuta sigara. Mwishowe niliacha kabisa.”

Je, Mungu anaweza kukusaidia ikiwa maombi yako yanapatana na mapenzi yake?

^ fu. 6 Yehova ni jina la Mungu kama linavyofunuliwa katika Biblia.