Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ufisadi Serikalini Utakwisha?

Je, Ufisadi Serikalini Utakwisha?

 Ufisadi wa maofisa wa serikali ni tatizo lililo ulimwenguni pote lenye madhara makubwa sana. a Kwa mfano, wakati wa janga la COVID-19, maofisa wa nchi moja baada ya nyingine walishtakiwa kwa kujitajirisha kwa pesa ambazo zilipaswa kutumiwa kusaidia watu wakabiliane na janga hilo. Kwa sababu ya ufisadi huo, watu wengi hawakupata matibabu waliyohitaji. Hivyo, watu waliteseka na hata kufa.

 Madhara ya ufisadi huu serikalini yako kila mahali. David Cameron, aliyekuwa waziri mkuu wa awali wa Uingereza, alisema hivi: “Ufisadi ni kama utando mkubwa wa buibui unaonasa nchi zote.”

 Hata hivyo, tuna uhakika kwamba ufisadi wote serikalini utakwisha. Kwa nini? Ona kile ambacho Biblia inasema Mungu atafanya.

Tunajuaje kwamba Mungu ataondoa ufisadi?

 Katika Biblia, Mungu anasema hivi: “Mimi, Yehova, ninapenda haki; Ninachukia unyang’anyi na ukosefu wa uadilifu.” b (Isaya 61:8) Watu wanapoteseka kwa sababu ya ufisadi wa wengine, Mungu anaona. (Methali 14:31) Anaahidi hivi: “Kwa sababu wale wanaoteswa wanakandamizwa, . . . nitainuka na kutenda.”​—Zaburi 12:5.

 Mungu atafanya nini? Badala ya kurekebisha serikali zilizopo, Mungu ataziondoa na kusimamisha ufalme wake unaoitwa, “Ufalme wa Mungu.” (Marko 1:14, 15; Mathayo 6:10) Biblia inasema hivi: “Mungu wa mbinguni atausimamisha ufalme ambao . . . utazipondaponda na kuzikomesha falme hizi [nyingine] zote, nao pekee utasimama milele.” (Danieli 2:44) Kwa kufanya hivyo, Mungu atakomesha ufisadi uliopo leo.

Serikali isiyo na ufisadi

 Tunajuaje kwamba Ufalme wa Mungu hautakuwa na ufisadi? Chunguza mambo yafuatayo.

  1.  1. Mamlaka. Ufalme unapata mamlaka yake kutoka kwa Mungu Mweza-Yote.​—Ufunuo 11:15.

     Kwa nini hilo ni muhimu: Serikali za wanadamu zinategemea pesa kutoka kwa wananchi ili kufanya utendaji wake. Mara nyingi, hilo hutokeza nafasi ya watu kupokea rushwa, kuiba, na kupotosha mambo. Hata hivyo, Ufalme huo unategemezwa na Mungu Mweza-Yote, basi siku zote utawaandalia raia wake kila kitu wanachohitaji.​—Zaburi 145:16.

  2.  2. Mtawala. Mungu amemweka Yesu Kristo kuwa mtawala wa Ufalme huo.​—Danieli 7:13, 14.

     Kwa nini hilo ni muhimu: Hata viongozi wazuri wanaweza kushawishiwa kufanya jambo baya. (Mhubiri 7:20) Tofauti na hilo, Yesu amethibitisha kwamba hawezi kuhongwa. (Mathayo 4:8-11) Isitoshe, anawapenda kikweli raia zake na anahangaikia hali yao.​—Zaburi 72:12-14.

  3.  3. Sheria. Sheria za Ufalme wa Mungu ni kamilifu, na wale wanaozitii wanapata furaha.​—Zaburi 19:7, 8.

     Kwa nini hilo ni muhimu: Mara nyingi, sheria zilizotungwa na wanadamu ni tata, zinalemea watu, na hazitekelezwi kwa njia inayofaa. Hivyo basi, sheria hizo hutokeza nafasi za watu kujihusisha katika ufisadi. Kwa upande mwingine, sheria za Mungu zina faida katika maisha ya kila siku. (Isaya 48:17, 18) Na si hilo tu, sheria za Mungu hazizingatii matendo yanayofanywa tu, bali pia kusudi la mtendaji. (Mathayo 22:37, 39) Bila shaka, Mungu anaweza kusoma mioyo na kuhakikisha kwamba sheria hizo zinatekelezwa kwa ufikirio.​—Yeremia 17:10.

 Tunakukaribisha ujifunze mengi zaidi kuhusu serikali ambayo haitakuwa na ufisadi iliyoahidiwa katika Biblia

a Kulingana na ufafanuzi fulani, neno “ufisadi” linamaanisha kutumia vibaya mamlaka ambayo mtu amepewa ili kujifaidi mwenyewe.

b Yehova ni jina la kibinafsi la Mungu. (Zaburi 83:18) Ona makala yenye kichwa “Yehova Ni Nani?”