Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Unapaswa Kuamini Utatu?

Unapaswa Kuamini Utatu?

Watu zaidi ya miliardi mbili ulimwenguni wanasema kwamba wao ni Wakristo. Wengi kati yao ni washiriki wa makanisa ambayo yanafundisha Utatu​—fundisho ambalo linasema kwamba Baba, Mwana, na roho mutakatifu wanafanyiza Mungu mumoja. Namna gani Utatu huo ulikuja kuwa fundisho kubwa la makanisa ya Kikristo? Jambo la maana zaidi, je, fundisho hilo linapatana na Biblia?

BIBLIA ilimalizika kuandikwa kati ya mwaka wa 1 na 100 kisha kuzaliwa kwa Yesu. Zaidi ya miaka 200 kisha hapo, ni kusema, katika mwaka wa 325 kisha kuzaliwa kwa Yesu, mafundisho ambayo yaliongoza kwenye fundisho la Utatu yalianza kutangazwa waziwazi kwenye mukutano wa maaskofu uliofanywa katika muji wa Nisea huko Asia ndogo, leo muji huo unaitwa Izniki, na unapatikana huko Uturuki. Kulingana na kitabu kimoja (New Catholic Encyclopedia), fundisho ambalo linasemekana lilianzishwa na Baraza la Nisea lilitoa maelezo ya kwanza ya mafundisho ya kanisa, kutia ndani maelezo kuhusu Mungu na Kristo. Hata hivyo, sababu gani lilionekana kuwa jambo la lazima kutoa maelezo kuhusu Mungu na Kristo mamia ya miaka kisha Biblia kumalizwa kuandikwa? Je, Biblia haieleze waziwazi habari hizo za maana juu ya Mungu na Kristo?

JE, YESU NI MUNGU?

Wakati Constantino aliwekwa kuwa mutawala pekee wa Utawala wa Roma, wale waliojiita kuwa Wakristo walikuwa na mawazo yenye kupingana juu ya uhusiano kati ya Mungu na Kristo. Je, Yesu alikuwa Mungu? Ao aliumbwa na Mungu? Ili kumaliza ubishi huo, Constantino aliwakusanya viongozi wa kanisa huko Nisea, si kwa sababu ya kutafuta ukweli wa kidini, lakini kwa sababu hakupenda utawala wake ugawanyike kwa sababu ya mambo ya dini.

‘Kwetu sisi kuna Mungu mumoja aliye Baba.’​—1 Wakorintho 8:6

Constantino aliwaomba maaskofu, ambao labda walikuwa mamia, wakubaliane juu ya jambo moja, lakini ombi lake halikuwa na matokeo mazuri. Kwa hiyo, akapendekeza kwamba baraza likubali fundisho lisiloeleweka la kwamba Yesu na Baba yake walikuwa “wa asili moja,” (homoousios), ni kusema, kitu kimoja. Neno hilo la falsafa (filozofia) ya Kigiriki lisilopatana na Biblia lilikuwa ndio mwanzo wa fundisho la Utatu ambalo lilikuja kuingizwa baadaye katika mafundisho ya kanisa. Bila shaka, mwisho wa miaka kati ya 301 na 400, fundisho la Utatu lilikuwa sasa na sehemu ya tatu ya kichwa cha mungu wa utatu, inayoitwa roho mutakatifu, kama linavyofundishwa leo.

SABABU GANI UNAPASWA KUCHUNGUZA FUNDISHO HILO?

Yesu alisema kwamba ‘waabudu wa kweli watamuabudu Baba katika kweli.’ (Yohana 4:23) Kweli hiyo imeandikwa katika Biblia. (Yohana 17:17) Je, Biblia inafundisha kwamba Baba, Mwana, na roho takatifu ni watu watatu katika Mungu mumoja?

Jambo moja ni kwamba, hakuna neno “Utatu” katika Biblia. Jambo lingine ni kwamba, hakuna siku Yesu alisema kuwa yeye analingana na Mungu. Lakini, Yesu aliabudu Mungu. (Luka 22:41-44) Jambo la tatu linahusu uhusiano wa Yesu na wafuasi wake. Hata kisha kufufuliwa na kuenda mbinguni, Yesu aliwaita wafuasi wake “ndugu zangu.” (Mathayo 28:10) Je, wafuasi wake hao walikuwa ndugu za Mungu Mweza-Yote? Hapana kabisa! Lakini kupitia imani yao katika Kristo, ni kusema, Mwana wa Mungu ambaye ana cheo kikubwa, wao pia walikuwa sasa wana wa Baba mumoja. (Wagalatia 3:26) Linganisha maandiko mengine na maneno yanayofuata ambayo yanatokana na fundisho ambalo linasemekana kuwa lilianzishwa na Baraza la Nisea.

Mambo ambayo Baraza la Nisea linasema juu ya Utatu:

“Tunaamini . . . Bwana mumoja Yesu Kristo . . . ambaye ni wa asili ya Baba, Mungu wa Mungu, Mwangaza wa Mwangaza, Mungu wa kweli wa Mungu wa kweli.”

Mambo ambayo Biblia inasema:

  • ‘Baba ni mukubwa kuliko mimi [Yesu].’​—Yohana 14:28. *

  • “Mimi [Yesu] ninapanda kwenda kwa Baba yangu na Baba yenu na kwa Mungu wangu na Mungu wenu.”​—Yohana 20:17.

  • ‘Kwetu sisi kuna Mungu mumoja aliye Baba.’​—1 Wakorintho 8:6.

  • “Abarikiwe Mungu na Baba ya Bwana wetu Yesu Kristo.”​—1 Petro 1:3.

  • “Mambo anayosema Amina [Yesu], . . . mwanzo wa uumbaji wa Mungu.”​—Ufunuo 3:14. *

^ Italiki ni zetu. Maandiko yote yanayotajwa katika habari hii yanatoka katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

^ Kitabu kinachosaidia kujifunza Biblia chenye kichwa Biblia Inafundisha Kabisa Nini? kina sura 19, kati ya sura hizo kuna sura hizi mbili: “Biblia Inafundisha Nini juu ya Mungu?” na “Yesu Kristo Ni Nani?” Mashahidi wa Yehova wanaweza kukupatia kopi ya kitabu hicho ao unaweza kukisoma kwenye adresi yetu ya Internete www.mt1130.com.