Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Kutafuta Wachawi Katika Ulaya

Kutafuta Wachawi Katika Ulaya

MAMIA ya miaka iliyopita katika Ulaya, kuogopa uchawi kulisukuma watu watafute wachawi na kuwaua. Jambo hilo lilifanyika sana katika inchi ya Ufaransa, Ujerumani, kaskazini mwa Italia, Usuisi, na Inchi za Chini, ni kusema, Ubelgiji, Lasembagi (Luxembourg), na Uholanzi. Kitabu kimoja kinasema hivi: “Makumi ya maelfu ya watu katika Ulaya na inchi zilizotawaliwa na Ulaya walikufa,” na “mamilioni mengine ya watu waliteswa, walifungwa, walisambishwa, walichukiwa, walihukumiwa kuwa na kosa, ao kuogopwa.” (Witch Hunts in the Western World) * Uoga huo ulianza namna gani? Ni nini iliyouchochea?

Mahakama ya Kuwahukumu Watu Walioasi Dini ya Katoliki na Kitabu The Hammer of Witches

Jambo lenye hatuwezi kukosa kuzungumuzia katika habari hii ni Mahakama za Kuwahukumu Watu Walioasi Dini ya Katoliki. Kitabu Der Hexenwahn (Kupenda Uchawi) kinaeleza kwamba mahakama hiyo iliundwa na Dini ya Katoliki ya Roma kati ya mwaka wa 1201 na 1300 “ili kugeuza watu wasioamini kwamba kuna Mungu na kuwazuia wengine wasianguke.” Mahakama hiyo ilitumika kwa ajili ya kanisa kama vile polisi.

Tarehe 5 mwezi wa 12, 1484, Papa Innocent wa 8 alitoa amri ya kipapa, ao hati, iliyokataza uchawi. Aliruhusu pia wapelelezi wawili wapiganishe tatizo hilo, wapelelezi hao ni Jakob Sprenger na Heinrich Kramer (anayejulikana pia kwa jina lake la Kilatini, Henricus Institoris). Wanaume hao wawili walitokeza kitabu chenye kichwa Malleus Maleficarum, ao The Hammer of Witches. Wakatoliki na Waprotestanti walikubali kitabu hicho kuwa chenye uwezo juu ya uchawi. Kitabu hicho kilikuwa na habari za kuwazia tu juu ya wachawi zenye kutegemea desturi za watu, kilionyesha mawazo ya kiteolojia na ya kisheria yaliyopinga uchawi, na kilitoa miongozo juu ya namna ya kutambua na kumaliza wachawi. Kitabu The Hammer of Witches kilielezwa kuwa ndicho kitabu “chenye ukatili mwingi na . . . chenye kuharibu sana kati ya vitabu vyote duniani.”

Kitabu The Hammer of Witches kilielezwa kuwa ndicho kitabu “chenye ukatili mwingi na . . . chenye kuharibu sana kati ya vitabu vyote duniani”

Mutu alishitakiwa hata ikiwa hakuwa na ishara yoyote iliyomutambulisha kuwa muchawi. Kitabu Hexen und Hexenprozesse (Uchawi na Kuwasambisha Wachawi) kilisema kwamba masambo “yalikuwa tu na kusudi la kumufanya mutu aliyeshitakiwa atubu, kupitia ushawishi, mukazo, ao nguvu.” Ilikuwa kawaida kuwatesa watu.

Kwa sababu ya kitabu The Hammer of Witches na amri iliyotolewa na Papa Innocent wa 8, wachawi walianza kutafutwa sana katika Ulaya. Zaidi ya hayo, mahakama hiyo ilisaidiwa na teknolojia mupya, ni kusema, mashini ya kuchapisha, yenye ilisaidia ili kueneza uoga juu ya uchawi, hata katika Atlantiki kufikia Amerika.

Ni Nani Walioshitakiwa?

Watu wengi walioshitakiwa, ni kusema, 70 juu ya 100 walikuwa wanawake, zaidi sana wajane, wenye hawakuwa na mutu wa kuwasemea. Watu hao walitia ndani pia maskini, wazee-wazee, na wanawake waliokuwa wanatunza kupitia majani, zaidi sana ikiwa dawa zao hazikusaidia watu. Hakuna mutu mwenye hangeshitakiwa, iwe tajiri ao maskini, mwanaume ao mwanamuke, mutu wa hali ya chini ao mutu anayejulikana sana.

Watu waliowaziwa kuwa wachawi walishitakiwa kila namna ya mambo mabaya. Gazeti moja la Ujerumani lilisema kwamba inawezekana “walileta baridi kali na mapigo ya konokono na viwavi ili kuharibu mbegu na matunda kwenye dunia.” (Damals) Ikiwa upepo mukali uliharibu mimea, ikiwa ngombe alishindwa kutoa maziwa, ikiwa mwanaume ao mwanamuke hana uwezo wa kuzaa, watu walisema kuwa ni kosa la wachawi!

Watu waliowaziwa kuwa wachawi walipimwa uzito kwa sababu watu waliwaza kuwa wachawi wana uzito kidogo ao hawana uzito

Namna gani wachawi walitambuliwa? Watu fulani walioshakiwa kuwa ni wachawi walifungwa na kutiwa ndani ya maji ya baridi “yaliyobarikiwa.” Wale waliozama walionwa kuwa si wachawi na waliondolewa katika maji hayo. Wale walioelea juu ya maji walionwa kuwa ni wachawi na waliuawa palepale ao walipelekwa kwenye mahakama ili kusambishwa. Wengine waliowaziwa kuwa wachawi walipimwa uzito kwa sababu watu waliwaza kwamba wachawi wana uzito kidogo ao hawana uzito.

Kitabu kingine kinasema kwamba namna nyingine ya kupima ikiwa mutu ni muchawi ilikuwa kutafuta “alama ya Shetani,” ni kusema, “ishara fulani inayoweza kuguswa iliyoachwa na Shetani kwa sababu ya mapatano yake na muchawi.” (Witch Hunts in the Western World) Maofisa walitafuta ishara hiyo “kwa kukata nywele zote za mutu aliyeshitakiwa na kuchunguza kila sehemu ya mwili,” mbele ya watu wengi! Kisha hapo, waliingiza sindano katika alama waliyopata, kama vile alama ya kizalikio, vipele, na makovu. Ikiwa mutu hakusikia maumivu ao kutokwa damu, alama hiyo ilionwa kuwa alama ya Shetani.

Dini ya Katoliki na ya Kiprotestanti, zote mbili zilichochea kutafuta wachawi, na katika maeneo fulani viongozi wa Waprotestanti walikuwa wakali sana kuliko wenzao Wakatoliki. Hata hivyo, baadaye, watu walianza kuwa na mawazo mengine. Kwa mufano, katika mwaka wa 1631, Friedrich Spee, padiri Mujesuti aliyekuwa amepeleka watu wengi ili waunguzwe kwenye muti wakiwa wazima kwa sababu “walihukumiwa kuwa wachawi,” aliandika kwamba kwa maoni yake hakuna hata mumoja kati yao aliyekuwa na kosa. Na alionya kwamba, ikiwa wataendelea kutafuta wachawi, inchi ingebaki bila mutu! Wakati huohuo, waganga walianza kutambua kwamba mambo kama vile kifafa ni tatizo la afya wala si kushikwa na roho waovu. Kati ya mwaka wa 1601 na 1700, hesabu ya watu walioshitakiwa kuwa wachawi ilipunguka kwa gafula, na kwenye mwisho wa miaka hiyo mia moja, hakuna mutu aliyeshitakiwa tena kuwa muchawi.

Kipindi hicho kibaya kinatufundisha nini? Jambo kubwa tunalojifunza ni hili: Watu wanaojiita kuwa Wakristo walileta maovu mengi sana wakati waliacha mafundisho safi ya Yesu Kristo na kuanza kufundisha uongo wa kidini na pia mambo yasiyo ya kweli yanayohusiana na desturi za mababu. Biblia ilitabiri mambo yenye kuleta haya yenye yangeingizwa katika Ukristo wa kweli kupitia watu wasiokuwa waaminifu. Juu ya jambo hilo Biblia ilionya hivi: “Ile njia ya kweli itatukanwa.”—2 Petro 2:1, 2.

^ Inchi zilizotawaliwa na Ulaya zilitia ndani inchi za Amerika.