Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Ikiwa Unafiwa na Bibi ao Bwana

Ikiwa Unafiwa na Bibi ao Bwana

BIBLIA inasema waziwazi kwamba mume anapaswa ‘kumupenda muke wake kama vile anavyojipenda mwenyewe.’ Na muke vilevile anapaswa ‘kumuheshimu sana mume wake.’ Wote wanapaswa kuishi kama ‘mwili mumoja.’ (Efe. 5:33; Mwa. 2:23, 24) Kadiri muda unavyopita, kifungo cha ndoa kinakuwa nguvu na bibi na bwana wanaendelea kupendana hata zaidi. Wanakuwa kama mizizi ya miti miwili inayokomalia pamoja. Bibi na bwana walio katika ndoa yenye furaha wanajisikia kuwa wanakaribiana sana katika kila jambo.

Lakini namna gani ikiwa bibi ao bwana anakufa? Wakati huo, kifungo hicho chenye nguvu cha maisha kinavunjika. Mara nyingi yule aliyefiwa na bibi ao bwana anaumia moyoni, anajisikia kuwa peke yake, na anaweza hata kuwa na hasira ao kufikiri kwamba ni kosa lake. Daniella aliyefanya miaka 58 katika ndoa, alikuwa akiona watu wengi waliofiwa na bibi ao bwana zao. * Lakini, bwana yake alipokufa, alisema hivi: “Sasa ndio ninaelewa uchungu wa kufiwa na bwana. Hauwezi kuelewa kabisa uchungu huo kama haujafikiwa na hali hiyo.”

NI KAMA UCHUNGU USIO NA MWISHO

Utafiti fulani umeonyesha kwamba hakuna jambo linalouma sana kama kupoteza bibi ao bwana uliyekuwa unapenda. Wengi ambao wamekwisha kufiwa na bibi ao bwana wanakubaliana na wazo hilo. Millie alifiwa na bwana miaka mingi iliyopita. Anapoeleza maisha yake ya ujane, anasema hivi: “Najisikia kuwa mwenye kupondekana sana.” Alisema hivyo alipokuwa akizungumuzia uchungu aliokuwa nao kisha kufiwa na bwana yake ambaye waliishi naye miaka 25 iliyopita.

Suzana alikuwa anafikiri kwamba wajane wanaoendelea kulilia bwana zao hata kisha miaka mingi, wanaonyesha uchungu unaovuka mipaka. Kisha, miaka 38 ya ndoa, bwana yake alikufa. Miaka 20 kisha kifo cha bwana yake, Suzana alisema hivi: “Ninaendelea kumukumbuka kila siku.” Analia kila mara anapomukumbuka.

Biblia inaonyesha kwamba kufiwa na bibi ao bwana kunaumiza sana na uchungu huo hauwezi kuisha mara moja. Sara alipokufa, Abrahamu, bwana yake, ‘aliingia ndani kumuombolezea na kumulilia.’ (Mwa. 23:1, 2) Ijapokuwa Abrahamu alikuwa na imani katika ufufuo, alihuzunika sana mupenzi wake alipokufa. (Ebr. 11:17-19) Kisha kifo cha bibi yake mupendwa Raheli, Yakobo aliendelea kumukumbuka. Aliendelea kuelezea wana wake kumuhusu Raheli.​—Mwa. 44:27; 48:7.

Mifano hiyo ya Biblia inatufundisha nini? Mara nyingi, mutu anapofiwa na bibi ao bwana yake anaendelea kusikia uchungu kwa miaka mingi. Hatupaswe kuona machozi na huzuni yake kama uzaifu, lakini tujue kwamba hayo ni matokeo ya jambo mbaya sana lililomufikia, ni kusema, kufiwa na bibi ao bwana yake mupendwa. Anapenda tujitie pa nafasi yake na kuendelea kumutegemeza.

TUSIHANGAIKIE SANA MAMBO YA KESHO

Maisha ya mujane hayamaanishe kwamba anarudia tena museja. Kisha kufanya miaka mingi katika ndoa, bwana anajua namna ya kumutia moyo bibi yake na kumufariji anapovunjika moyo. Bwana yake anapokufa, hilo linamaanisha kwamba mutu aliyemupenda na kumufariji haiko tena. Vilevile, kisha kuishi naye kwa miaka mingi, bibi anajua namna ya kumufanya bwana yake ajisikie salama na mwenye furaha. Hakuna jambo linaloshinda kumugusa kwa upendo, kumuambia maneno yenye kumufariji, kuhangaikia mahitaji yake. Bibi yake anapokufa, bwana anaweza kujisikia kuwa peke yake katika maisha. Kwa hiyo, watu fulani ambao wamefiwa na bibi ao bwana wanaogopa na kujiuliza maulizo mengi kuhusu wakati ujao. Ni kanuni gani ya Biblia inayoweza kuwasaidia wajisikie kuwa na amani na usalama?

Mungu anaweza kukusaidia usihangaikie sana mambo ya kesho unapopambana na uchungu wa kufiwa na bibi ao bwana

‘Musihangaike kamwe juu ya kesho, kwa maana kesho itakuwa na mahangaiko yake yenyewe. Unatosha kila siku ubaya wake.’ (Mt. 6:34) Maneno hayo ya Yesu yanatumiwa zaidi sana kuhusiana na mahitaji ya kimwili, lakini yamesaidia wengi wavumilie jaribu la kufiwa na mupendwa. Miezi fulani kisha kufiwa na bibi, mujane mumoja anayeitwa Charles aliandika hivi: “Ningali ninateseka sana ninapomukumbuka Monique na wakati fulani inaonekana kwamba huzuni yangu inaongezeka hata zaidi. Lakini, nimetambua kwamba hilo ni jambo la kawaida na mwishowe uchungu wangu utapunguka kadiri wakati unavyopita.”

Bila shaka, Charles alipaswa kuvumilia kadiri “miaka ilivyopita.” Ni jambo gani lilimusaidia avumilie? Alisema hivi: “Kwa musaada wa Yehova, sihangaikie sana mambo ya kesho.” Charles hakulemewa na huzuni. Uchungu wake haukuisha mara moja, lakini haukumufanya akose tumaini. Ikiwa umefiwa na bibi ao bwana, jikaze kutokuhangaikia sana mambo ya kesho. Haujue baraka ao kitia-moyo gani ambacho utapata kesho.

Yehova hakumuumba mwanadamu ili akufe. Tofauti na hilo, kifo ni moja kati ya “kazi za Ibilisi.” (1 Yoh. 3:8; Rom. 6:23) Shetani anatumia kifo na woga unaoletwa na kifo ili kufanya watu wengi wawe watumwa na kuwafanya wakose tumaini. (Ebr. 2:14, 15) Shetani anafurahi wakati mutu fulani anafikiri kama haiwezekani kuwa na furaha ya kweli na kutosheka leo, na hata katika ulimwengu mupya wa Mungu. Kwa hiyo, uchungu mukubwa ambao mutu anasikia anapofiwa na bibi ao bwana yake ni matokeo ya zambi ya Adamu na uasi wa Shetani. (Rom. 5:12) Yehova ataondoa mateso yote na kuangamiza silaha ya Shetani inayoumiza sana, ni kusema, kifo. Kati ya wale ambao wamekombolewa katika utumwa wa Shetani kuna pia watu wengi ambao wamefiwa na bibi ao bwana, kama vile wewe.

Ufufuo utatokeza mabadiliko mengi katika familia ya kibinadamu. Wazia tate ao nkambo na wazee wengine wa ukoo watakaofufuliwa na kufikia polepole ukamilifu pamoja na watoto wao na watoto wa watoto wao. Uzee utaondolewa kabisa. Je, vijana watajifunza kuona wazee wa ukoo tofauti na namna wanavyowaona leo? Je, hatutumaini kwamba mabadiliko hayo yatasaidia kufanya watu wawe na uhusiano muzuri?

Tunaweza kuwa na maulizo mengi kuhusu wale watakaofufuliwa. Kwa mufano, itakuwa namna gani kwa wale waliofiwa na bibi ao bwana wawili ao zaidi? Siku moja, Masadukayo walimuuliza Yesu kuhusu mwanamuke aliyefiwa na bwana yake wa kwanza, kisha bwana wa pili mupaka kufikia bwana wa saba. (Lu. 20:27-33) Wote hao watakuwa na uhusiano gani wakati wa ufufuo? Hatujue, na hakuna sababu ya kuwazia​-wazia mambo kuhusu jambo hilo ao kujisumbua kuhusu mambo hayo ambayo hatujue. Tumutegemee tu Mungu. Ukweli ni kwamba, kila jambo ambalo Yehova atafanya wakati ujao litakuwa nzuri; hatuna sababu ya kuogopa.

TUMAINI LA UFUFUO LINATUFARIJI

Moja kati ya mafundisho yaliyo wazi zaidi ya Neno la Mungu ni kwamba wapendwa wetu waliokufa watafufuliwa. Habari za Biblia kuhusu ufufuo mbalimbali uliotendeka wakati uliopita zinatuhakikishia kwamba “wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti [ya Yesu] na kutoka.” (Yoh. 5:28, 29) Wale watakaokuwa wazima wakati huo watafurahia kukutana na wale watakaofufuliwa. Kwa upande mwingine, hatuwezi kabisa kuwazia furaha ambayo wale watakaofufuliwa watakuwa nayo.

Wafu watakapokuwa wakifufuliwa, kutakuwa shangwe kubwa ambayo haijapata kuwa duniani. Mamilioni ya watu waliokuwa wamekufa wataishi tena pamoja na wanadamu wengine. (Mk. 5:39-42; Ufu. 20:13) Kutafakari juu ya muujiza huo wa wakati ujao kunaweza kufariji wote ambao wamefiwa na wapendwa wao.

Je, kutakuwa sababu ya kuhuzunika wakati jambo hilo litatendeka? Hapana. Isaya 25:8 inaonyesha kwamba Yehova “kwa kweli atameza kifo milele.” Hilo linatia ndani kumaliza kabisa uchungu wote unaotokana na kifo, kwa sababu unabii huo unaendelea kusema hivi: “Bwana Mwenye Enzi Kuu Yehova hakika atafuta machozi katika nyuso zote.” Ikiwa una huzuni sasa kwa sababu bibi ao bwana yako amekufa, bila shaka ufufuo utakufurahisha.

Hakuna mwanadamu anayeelewa vizuri kabisa mambo yote ambayo Mungu atatimiza katika ulimwengu mupya. Yehova anasema hivi: “Kama vile mbingu zilivyo juu kuliko dunia, ndivyo njia zangu zilivyo juu kuliko njia zenu, na mawazo yangu kuliko mawazo yenu.” (Isa. 55:9) Ahadi ya Yesu kuhusu ufufuo unaokuja inatutolea nafasi ya kumutumainia Yehova kama vile Abrahamu alivyofanya. Jambo la maana kwa kila Mukristo leo ni kufanya mapenzi ya Mungu ili ‘kuhesabiwa kustahili kupata ule mufumo wa mambo’ pamoja na wale watakaofufuliwa.​—Lu. 20:35.

SABABU YA KUWA NA TUMAINI

Kuliko kukata tamaa, endelea kuwa na tumaini. Kwa maoni ya kibinadamu, hakuna jambo la kutumainia wakati ujao. Lakini Yehova ametutolea tumaini nzuri. Hatuwezi kujua kwa uhakika kabisa namna Yehova atakavyotosheleza mahitaji na tamaa zetu, lakini tunapaswa kuwa hakika kwamba atafanya hivyo. Mutume Paulo aliandika hivi: ‘Tumaini linaloonekana si tumaini, kwa maana mutu anapoona kitu, je, yeye hukitumainia? Lakini tukitumainia kile ambacho hatuone, sisi huendelea kukingojea kwa uvumilivu.’ (Rom. 8:24, 25) Kutumainia kabisa ahadi za Mungu kutakusaidia kuvumilia. Ukivumilia, utakuwa na wakati ujao ulio muzuri sana; na wakati huo Yehova “atakupa maombi ya moyo wako.” Atatosheleza “tamaa ya kila kitu kilicho hai.”​—Zab. 37:4; 145:16; Lu. 21:19.

Tumainia ahadi ya Yehova ya wakati ujao wenye kujaa shangwe

Yesu alipokuwa karibu kufa, mitume wake walisumbuka sana. Yesu aliwafariji kwa maneno haya: “Mioyo yenu isitaabike. Iweni na imani katika Mungu, iweni na imani pia katika mimi.” Aliwaambia hivi: “Sitawaacha ninyi mayatima. Nitakuja kwenu.” (Yoh. 14:1-4, 18, 27) Maneno hayo yangesaidia wafuasi wake watiwa-mafuta katika miaka iliyofuata ili wawe na tumaini na wavumilie. Vivyo hivyo, wale wanaongojea kwa hamu kuona wapendwa wao wakati wa ufufuo hawana sababu ya kukata tamaa. Yehova na Mwana wake hawatawasahau. Uwe hakika na jambo hilo!

^ Majina yamebadilishwa.