Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Alipendwa na Mungu na Rafiki Zake Pia

Alipendwa na Mungu na Rafiki Zake Pia

Wafundishe Watoto Wako

Alipendwa na Mungu na Rafiki Zake Pia

HAKUNA mtu anayejua jina lake leo. Anajulikana tu kwa jina la baba yake, Yeftha. Acha tuchunguze katika Biblia na kujifunza kuhusu watu hao wawili. Tutaona kuwa binti ya Yeftha alipendwa na Mungu na rafiki zake pia.

Tunaweza kusoma kumhusu Yeftha na binti yake kwenye Biblia katika kitabu cha Waamuzi sura ya 11. Kwa kuwa Yeftha alikuwa mtumishi mwaminifu wa Mungu, hapana shaka kwamba alizungumzia Maandiko kwa ukawaida pamoja na binti yake.

Yeftha aliishi kabla ya watu wa Mungu, Waisraeli, kuomba kuwa na mfalme wa kibinadamu awatawale. Yeftha alikuwa mwanamume mwenye nguvu na uwezo wa kupigana. Hivyo, Waisraeli wakamwomba awaongoze katika pigano lao dhidi ya Waamoni, taifa jirani ambalo lilikuwa likipigana na Waisraeli.

Yeftha alitaka Mungu amsaidie kuwashinda Waamoni, hivyo akaweka ahadi. Yeftha alisema kwamba ikiwa Yehova atamsaidia kushinda, atampa mtu wa kwanza atakayetoka katika nyumba yake wakati atakaporudi nyumbani. Mtu huyo angetumika miaka yake yote katika hema la kukutania la Mungu—mahali ambapo watu walikuwa wakimwabudu Mungu wakati huo. Je, unajua ni nani aliyetoka nje kwanza? *

Ndiyo, ni binti ya Yeftha! Yeftha alihuzunika sana. Alikuwa na mtoto mmoja tu. Lakini alikuwa ametoa ahadi kwa Yehova na alipaswa kuitimiza. Mara moja, binti yake akasema: “Baba yangu, ikiwa umemfungulia Yehova kinywa chako, nitendee kulingana na neno lililotoka katika kinywa chako.” Kisha, akaomba aruhusiwe kwenda milimani kwa miezi miwili ili akaomboleze. Kwa nini alikuwa na huzuni hivyo? Kwa sababu kwa kutimiza ahadi ya baba yake, alikuwa anapoteza haki yake ya kuolewa na kupata watoto. Hata hivyo, hakuona tamaa zake kuwa jambo la maana. Alitaka kumtii baba yake na kuwa mshikamanifu kwa Yehova. Je, unafikiri alimfurahisha Yehova na baba yake?

Hivyo, Yeftha akamruhusu binti yake aende milimani kwa miezi miwili akiwa na rafiki zake. Aliporudi, baba yake alitimiza ahadi yake kwa kumpeleka katika hema la kukutania huko Shilo, akaishi huko maisha yake yote. Kila mwaka mabinti wa Israeli walienda Shilo na kumtia moyo binti ya Yeftha.

Je, unawajua watoto wanaowatii wazazi wao na kumpenda Yehova pia?— Ni vema kuwajua watoto hao vizuri na kuwa rafiki zao. Ikiwa utamwiga binti ya Yeftha na kuwa mtiifu na mshikamanifu, utakuwa na rafiki wazuri. Utawafurahisha wazazi wako, na Yehova atakupenda pia.

Soma katika Biblia yako

Kumbukumbu la Torati 6:4-6

Waamuzi 11:30-40

1 Wakorintho 7:37, 38

[Maelezo ya Chini]

^ Kama unasoma sehemu hii pamoja na mtoto, unapoona kistari kama hiki (—), tua na umtie moyo mtoto atoe maoni yake.