Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

Jina la Mungu Limejulishwa Katika Luga ya Kiswahili

Jina la Mungu Limejulishwa Katika Luga ya Kiswahili

Jina la Mungu Limejulishwa Katika Luga ya Kiswahili

Watu wengi wanaposikia neno “Kiswahili” mara moja wanafikiria Afrika na misitu yake ya Serengeti iliyo na wanyama wengi wanaozunguka​-zunguka ndani. Lakini, kuna mambo mengi ya kujifunza juu ya luga ya Kiswahili na watu wanaozungumuza luga hiyo.

KISWAHILI ni luga inayozungumuzwa na watu zaidi ya milioni 100 katika inchi karibu 12 za Afrika ya kati na ya mashariki. * Serikali ao guvernema ya inchi nyingi kama vile Kenya, Tanzania, na Uganda zimefanya Kiswahili kuwa luga ya taifa ao ya serikali. Na katika inchi jirani za inchi hizo tatu, luga ya Kiswahili inazungumuzwa na watu wengi, na hivyo inasaidia watu wa maeneo hayo mbalimbali kufanya biashara na kupashana habari kwa vyepesi.

Luga ya Kiswahili imesaidia sana kuunganisha watu wa Afrika ya Mashariki. Kwa mufano, katika Tanzania tu, watu wanazungumuza luga za kabila karibu 114. Wazia unasafiri kilometre 40 mupaka 80 tu kutoka nyumbani kwako, unakutana na watu wanaozungumuza luga tofauti kabisa na luga yako! Na tuseme nini ikiwa unakuta kila kijiji kidogo kina luga yake? Namna gani utazungumuza na watu hao? Mufano huo unatusaidia kuelewa faida ya kuzungumuza luga moja.

Historia ya Luga ya Kiswahili

Inajulikana kama watu walianza kusema luga ya Kiswahili tangu miaka ya 900 hivi, na walianza kuiandika katika miaka ya 1500. Wale wanaojifunza Kiswahili wanafikia kuvumbua mara moja kama maneno mengi yanafanana na Kiarabu. Karibu 20% ya maneno ya Kiswahili ilitokana na Kiarabu, na 80% ilitokana na luga zingine za Afrika. Kwa hiyo, si jambo la kushangaza kwamba Kiswahili kilikuwa kinaandikwa katika alfabeti ya Kiarabu kwa miaka mingi.

Leo, Kiswahili kinaandikwa katika alfabeti ya Kiroma. Sababu gani kumekuwa badiliko hilo? Ili kupata jibu, turudi kwanza nyuma katikati ya miaka ya 1800, wakati wamisionere wa kwanza​-kwanza wa Ulaya walifika katika inchi za Mashariki mwa Afrika, wakiwa na kusudi la kuhubiria wakaaji wa inchi hizo ujumbe wa Biblia.

Neno la Mungu Linafika kwa Mara ya Kwanza Katika Inchi za Mashariki mwa Afrika

Katika mwaka wa 1499, Vasco de Gama alifanya safari yake katika sehemu za kusini za Afrika, wakati huo wamisionere wa Portugal waliingiza dini ya Kikatoliki katika Sehemu za Mashariki za Afrika kwa kujenga parokia yao huko Zanzibar. Lakini, kisha miaka 200, wakaaji wa Zanzibar wakakataa dini ya Kikatoliki na wakawafukuza wamisionere hao waliotoka Portugal.

Kisha miaka 150, misionere wa Alemanye anayeitwa Johann Ludwig Krapf alileta tena Neno la Mungu katika Afrika ya Mashariki. Alipofika huko Mombasa, Kenya, katika mwaka wa 1844, wakaaji wa maeneo yaliyo kandokando ya bahari walikuwa Waislamu, lakini wale waliokuwa katika maeneo mengine ya ndani waliendelea kushikilia imani zao za kienyeji na kuabudu mababu. Krapf aliona kama ilikuwa lazima watu wote wawe na Biblia.

Krapf hakupoteza wakati, alianza mara moja kujifunza luga ya Kiswahili. Mwezi wa 6, 1844, kisha tu kufika, alianza kazi ngumu ya kutafsiri Biblia. Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, mwezi uliofuata, bibi yake alikufa kisha miaka miwili ya ndoa, kisha siku chache mutoto wao mwanamuke pia akakufa. Ijapokuwa alihuzunika sana, aliendelea na kazi yake ya kutafsiri Biblia. Katika mwaka wa 1847, sura tatu za kwanza za kitabu cha Mwanzo zikachapishwa katika luga ya Kiswahili; hiyo ndiyo ilikuwa kazi ya kwanza ya kuchapisha Biblia katila luga ya Kiswahili.

Krapf ndiye mutu wa kwanza aliyetumia alfabeti ya Kiroma ili kuandika Kiswahili kuliko kutumia alfabeti ya Kiarabu ambayo watu walizoea kutumia. Krapf alitoa sababu nyingi zilizomuchochea aache kutumia alfabeti ya Kiarabu. Kati ya sababu hizo, alisema kama alfabeti ya Kiarabu ilikuwa ngumu kwa wamisionere wengine kutoka Ulaya ambao wangependa kujifunza luga hiyo baadaye, na kama alfabeti ya Kiroma ingewasaidia “Wakaaji wa Afrika wajifunze luga za Ulaya kwa vyepesi.” Watu wengine waliendelea kutumia alfabeti ya Kiarabu kwa miaka mingi; na sehemu fulani za Biblia ya Kiswahili zilichapishwa katika alfabeti hiyo ya Kiarabu. Kutumia alfabeti ya Kiroma kulisaidia kabisa watu wengi kujifunza Kiswahili kwa vyepesi. Kwa kweli, wamisionere wengi na watu wengine wanaojifunza Kiswahili wamefurahia sana badiliko hilo.

Kama tulivyoona, Krapf ndiye aliyekuwa mutu wa kwanza kutafsiri Neno la Mungu katika luga ya Kiswahili. Tena, aliwatayarishia njia watafsiri wengine waliokuja nyuma yake. Aliandika kitabu cha kwanza cha sarufi (grammaire) na pia kamusi katika luga hiyo.

Jina la Mungu Katika Luga ya Kiswahili

Krapf alipotafsiri sura tatu za kwanza za kitabu cha mwanzo, jina la Mungu lilitafsiriwa tu “Mungu Mweza-Yote.” Lakini, mwishoni mwa miaka ya 1800, watu wengine wengi walifika Mashariki mwa Afrika na waliendelesha kazi ya kutafsiri Biblia nzima katika luga ya Kiswahili. Kati yao kulikuwa Johann Rebmann, William Taylor, Harry Binns, Edward Steere, Francis Hodgson, na Arthur Madan.

Jambo la lazima ni kwamba katika tafsiri hizo za kwanza-kwanza za Biblia, watafsiri fulani waliliingiza jina la Mungu mahali pengi katika Maandiko yote ya Kiebrania! Watafsiri waliokuwa huko Zanzibar walilitafsiri jina la Mungu “Yahuwa,” na wale waliokuwa huko Mombasa walilitafsiri “Jehova.”

Katika mwaka wa 1895 hivi, Biblia nzima ilipatikana katika luga ya Kiswahili. Katika miaka iliyofuata, tafsiri zingine zilipatikana, hata kama hazikugabuliwa kwa uwingi. Mwanzoni mwa miaka ya 1900, kazi nyingi zilifanywa ili kuweka luga ya Kiswahili katika namna inayokubalika Mashariki mwa Afrika. Hilo likaleta matokeo mazuri: Kwanza, Biblia inayoitwa Swahili Union Version ikachapishwa katika mwaka wa 1952 na kuwa Biblia inayotumiwa na watu wengi katika sehemu hiyo ya Afrika. Na tena, jina “Yehova” likakubaliwa kuwa jina la Mungu katika luga ya Kiswahili.

Jambo la kuhuzunisha ni kwamba, tafsiri hizo za kwanza-kwanza zilipoacha kuchapishwa, jina la Mungu likaanza kupotea. Watafsiri fulani wa sasa wameliondoa kabisa jina la Mungu katika Biblia zao, na wengine wameliacha mahali pachache tu. Kwa mufano, katika tafsiri inayoitwa Union Version jina la Mungu lilipatikana ndani mara 15 tu, lakini tafsiri hiyo iliporekebishwa katika mwaka wa 2006, jina hilo lilipatikana ndani mara 11 tu. *

Hata ikiwa watafsiri wa Biblia hiyo wameliondoa jina la Mungu mahali pengi, kuna jambo fulani la lazima kuhusu tafsiri hiyo. Kwenye ukurasa wa kwanza, kuna maelezo yanayoonyesha waziwazi kama jina la Mungu ni Yehova. Hilo limewasaidia watu wengi wanaotafuta kweli wajue jina la pekee la Baba yetu wa mbinguni kupitia Biblia zao.

Lakini, kuna mambo mengine ya kujifunza juu ya historia ya luga ya Kiswahili. Katika mwaka wa 1996, Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ya Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo ilitolewa. Hiyo ndiyo tafsiri ya kwanza ya Kiswahili iliyorudisha jina la Yehova mara 237 kuanzia Mathayo mupaka Ufunuo. Kisha, katika mwaka wa 2003, Biblia nzima inayoitwa Biblia Takatifu​—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya ilitolewa. Mupaka leo, karibu Biblia 900 000 zimechapishwa katika luga ya Kiswahili.

Jina la Mungu halifichwe tena kwa kutumia majina ya cheo ao kuandikwa tu kwenye kurasa za kwanza​-kwanza za tafsiri fulani. Sasa, kila mara watu wenye nia nzuri wanapofungua Tafsiri ya Ulimwengu Mpya, wanamukaribia Yehova zaidi wanaposoma jina lake linalopatikana ndani zaidi ya mara 7 000.

Tena, tafsiri hiyo inatumia Kiswahili cha kisasa ambacho watu wote wanaozungumuza Kiswahili katika Afrika ya Mashariki wanaelewa kwa vyepesi. Zaidi ya hayo, imeondoa mawazo mengi ya uongo ambayo watafsiri wengi waliingiza katika maandiko. Kwa hiyo, musomaji anaweza kuwa hakika kama mambo anayosoma ni “maneno sahihi ya kweli” yaliyoongozwa na roho ya Yehova Mungu, Muumbaji wetu.​—Mhubiri 12:10.

Mashahidi wa Yehova wengi wameonyesha shukurani yao kwa ajili ya Tafsiri ya Ulimwengu Mpya. Vicent, Shahidi wa Yehova aliye na miaka 21 ambaye ni muhubiri wa wakati wote, alisema hivi: “Nilifurahi sana kwa sababu ya Kiswahili chepesi kinachotumiwa katika Tafsiri ya Ulimwengu Mpya na kwa sababu tafsiri hiyo imerudisha jina la Yehova mahali ambapo tafsiri zingine zililiondoa.” Frieda, mama wa watoto watatu, alisema kama tafsiri hiyo imefanya iwe vyepesi kwake kuwafasiria watu wengine mafundisho ya Biblia.

Kumepita miaka zaidi ya 150 tangu kazi ya kutafsiri Neno la Mungu katika luga ya Kiswahili ilipoanza. Yesu alisema kama ‘amelifunua jina la Baba yake.’ (Yohana 17:6) Sasa, Mashahidi wa Yehova zaidi ya 76000 wanaozungumuza Kiswahili katika Afrika ya kati na ya Mashariki, wanafurahia kusaidia watu wote kujua jina la Yehova kwa kutumia Tafsiri ya Ulimwengu Mpya.

[Maelezo ya chini]

^ Katika inchi hizo, watu wanazungumuza aina mbalimbali ya Kiswahili.

^ Linapatikana katika Mwanzo 22:14; Kutoka 6:2-8 (mara mbili); 17:15 (linaandikwa Yahweh); Waamuzi 6:24; Zaburi 68:20; 83:18; Isaya 12:2; 26:4; 49:14; na Yeremia 16:21.

[Karte kwenye ukurasa wa 26, 27]

(Ili kuona maelezo hayo, ona kitabu)

Inchi za Afrika Ambamo Kiswahili Kinazungumuzwa

Uganda

Kenya

Tanzania

Congo, Kinshasa

Rwanda

Burundi

Zanzibar

Zambie

Mozambique

Malawi

Soudan

Etiopia

Somalie

[Picha katika ukurasa wa 27]

Mwanzo 1:1-3 katika Tafsiri ya Kiswahili ya Johann Krapf, mwaka wa 1847

[Picha zimetolewa na]

Ilichukuliwa Katika Gazeti la American Oriental Society, Vol. 1, No. 3, 1847

[Picha katika ukurasa wa 28]

Sehemu ya Mathayo sura ya 1 katika Kiswahili cha alfabeti ya Kiarabu mwaka wa 1891

[Picha katika ukurasa wa 28]

Jina la Mungu, Yehova, kwenye ukurasa wa kwanza wa Biblia inayoitwa “Swahili Union Version”

[Picha katika ukurasa wa 28]

Jina la Mungu lilitafsiriwa “Yahuwa” na “Jehova” katika tafsiri za kwanza-kwanza

[Picha katika ukurasa wa 29]

Mashahidi wa Yehova wengi wanafurahia kutumia “Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya”

[Maneno ili kueleza mahali picha zilitokea, ukurasa wa 28]

Picha Zote: Bible Society of Tanzania na Bible Society of Kenya; juu kushoto: Image courtesy of the National Library of Scotland