Ona video zinazopatikana

Ona habari zilizo ndani

KICHWA: UFUFUO WA YESU UNA MAANA GANI KWAKO?

Je, Kweli Yesu—Alifufuliwa?

Je, Kweli Yesu—Alifufuliwa?

HÉRODOTE, mwanahistoria Mugiriki aliyeishi kumepita miaka 2500, alieleza historia juu ya Wamisri wa siku zake. Aliandika hivi: “Kwenye karamu za watu matajiri, kisha chakula cha muchana, mwanaume mumoja alileta sanamu ya muti ya maiti ya mutu ndani ya sanduku, ambalo lilichorwa na kupakwa rangi na lililokuwa na urefu wa mukono mumoja ao mikono miwili, sanduku hilo lilifanana kabisa na sanduku la kweli la maiti. Aliwaonyesha waalikwa wote sanduku hilo, na kusema, ‘Mukunywe na mufurahi, lakini mutazame sanduku hili; kwa sababu hivi ndivyo mutakavyokuwa wakati mutakufa.’”

Si Wamisri peke yao waliokuwa na maoni kama hayo juu ya maisha na kifo. Leo pia, maneno “Kula, kunywa, na ufurahi” ni maneno ambayo watu wanasema kwa ukawaida. Ikiwa mwisho wa maisha ni kifo, sababu gani usiyafurahie wakati ungali muzima? Kwa nini mutu ajikaze kufanya mambo yaliyo sawa? Ikiwa mwisho wa maisha ni kifo, basi ni vizuri kufurahia maisha sasa. Mutume Paulo alizungumuza kuhusu maoni hayo ya watu. Alieleza maoni ya watu ambao hawaamini kwamba kutakuwa ufufuo, alisema hivi: “Ikiwa wafu hawatafufuliwa, ‘na tule na tunywe, kwa maana kesho tutakufa.’”​—1 Wakorintho 15:32.

Bila shaka, Paulo mwenyewe hakuamini kama wafu watasahauliwa milele. Alisadiki kwamba wafu wataishi tena, wakiwa na tumaini la kutokufa tena. Usadikisho huo ulitegemea tukio la maana sana, ambalo aliona kuwa haliwezi kutiliwa shaka, ni kusema, ufufuo * wa Kristo Yesu. Kwa kweli, ufufuo huo lilikuwa tukio moja kubwa ambalo lilitia nguvu imani ya wanafunzi wa kwanza.

Hata hivyo, ufufuo wa Yesu una maana gani kwetu? Namna gani tunajua kwamba Yesu alifufuliwa kwelikweli? Acheni tuone namna Paulo alivyofikiri juu ya mambo hayo alipowaandikia Wakristo waliokuwa wakiishi huko Korintho.

INGEKUWA NAMNA GANI IKIWA KRISTO HAKUFUFULIWA?

Wakristo fulani katika muji wa Korintho wa zamani walivurugika juu ya wazo hilo la ufufuo, na wengine hawakuamini kabisa ufufuo wa wafu. Katika barua yake ya kwanza aliyowaandikia Wakristo wa muji huo wa Korintho, mutume Paulo alionyesha mambo ambayo yangetokea ikiwa ufufuo halikuwa jambo la kweli. Aliandika hivi: ‘Ikiwa, kwa kweli, hakuna ufufuo wa wafu, basi Kristo hakufufuliwa. Lakini ikiwa Kristo hakufufuliwa, hakika kuhubiri kwetu ni bure, na imani yetu ni bure. Zaidi ya hayo, tunaonekana pia kuwa mashahidi wa uongo wa Mungu . . . Imani yenu ni bure; ninyi bado muko katika zambi zenu. . . . Pia, wale waliolala usingizi katika kifo katika muungano na Kristo waliangamia.’​—1 Wakorintho 15:13-18.

‘Aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano kwa wakati mumoja . . . Baadaye alimutokea Yakobo, kisha mitume wote; lakini mwisho kabisa alinitokea mimi pia.’​—1 Wakorintho 15:6-8

Paulo alianza maneno yake kwa mawazo haya ambayo ni vigumu kuyapinga: Ikiwa wafu hawatafufuliwa, kwa hiyo, Kristo ambaye alikufa, hakufufuliwa. Ikiwa Kristo hakufufuliwa, matokeo yangekuwa nini? Hivyo, kuhubiri habari njema kungekuwa bure, uongo mutupu kabisa. Zaidi ya yote, ufufuo wa Kristo lilikuwa jambo la lazima sana katika imani ya Kikristo, jambo linalohusiana sana na mafundisho ya musingi ya Biblia juu ya utawala wa Mungu, jina lake, Ufalme wake, na ukombozi wetu. Ikiwa Yesu hakufufuliwa, ujumbe ambao Paulo na mitume wengine walihubiri haungekuwa na maana yoyote, yangekuwa maneno ya bure kabisa na yasiyofaa kitu.

Kungekuwa pia matokeo mengine. Ikiwa Kristo hakufufuliwa kutoka kwa wafu, imani ya Kikristo ingekuwa isiyofaa kitu, ya bure kabisa na inayotegemea uongo mutupu. Tena, Paulo na wengine wangekuwa wanahubiri mambo ya uongo juu ya ufufuo wa Yesu na pia juu ya yule ambaye walisema kwamba alimufufua Yesu, ni kusema, Yehova Mungu. Zaidi ya hayo, maneno Kristo ‘alikufa kwa ajili ya zambi zetu’ yangekuwa pia uongo, kwa sababu ikiwa Mukombozi mwenyewe hakuokolewa kutoka katika kifo, hangeweza kuwakomboa wengine. (1 Wakorintho 15:3) Hilo lingemaanisha kama Wakristo ambao kwa njia fulani walikufa kwa sababu ya imani yao, walikufa wakiwa na tumaini la uongo kwamba wangefufuliwa.

Paulo alimalizia kwa maneno haya: ‘Ikiwa ni katika maisha haya tu tumemutumaini Kristo, sisi ndio wa kusikitikiwa zaidi kati ya watu wote.’ (1 Wakorintho 15:19) Kama Wakristo wengine, Paulo alipatwa na hasara, aliteswa, alivumilia matatizo, na alipambana na kifo kwa sababu ya kuamini ufufuo na mambo yote ambayo ufufuo utawezesha. Maisha yangekuwa bure kabisa ikiwa tumaini la ufufuo lilikuwa la uongo!

SABABU GANI UNAPASWA KUAMINI UFUFUO?

Paulo hakuamini wazo lolote kati ya mawazo hayo yasiyo ya kweli. Alijua kwamba Yesu alifufuliwa kutoka kwa wafu, na aliwaonyesha Wakorintho kwa kifupi mambo yote yanayohakikisha kwamba Kristo alifufuliwa, ni kusema, ‘kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya zambi zetu kulingana na Maandiko; na kwamba alizikwa, ndiyo, kwamba alifufuliwa siku ya tatu kulingana na Maandiko; na kwamba alimutokea Kefa, kisha wale kumi na wawili.’ * Kisaha, Paulo anaongeza hivi: ‘Baadaye aliwatokea ndugu zaidi ya mia tano kwa wakati mumoja, ambao walio wengi kati yao wapo mupaka sasa, lakini wengine wamelala usingizi katika kifo. Baadaye alimutokea Yakobo, kisha mitume wote; lakini mwisho kabisa alinitokea mimi pia.’​—1 Wakorintho 15:3-8.

Paulo alianza kwa maneno yenye kusadikisha kwamba Kristo alikufa kwa ajili ya zambi zetu, alizikwa, na akafufuliwa. Ni nini kilimufanya Paulo awe na usadikisho huo? Sababu moja ilikuwa ni ushuhuda wa Mashahidi wengi waliomuona Yesu kisha kufufuliwa kwake. Kisha kufufuliwa kwake, Yesu aliwatokea watu mbalimbali (kati yao kuna Paulo mwenyewe), vikundi vidogo vidogo vya watu, na hata kikundi kikubwa cha watu 500, ambao wengi wao walikuwa na mashaka waliposikia habari za kwamba Yesu alifufuliwa! (Luka 24:1-11) Wengi wa wale waliomuona Yesu kisha kufufuliwa kwake walikuwa wangali wanaishi katika siku za Paulo na wangeweza kuulizwa ili kuhakikisha kwamba Yesu aliwatokea watu mbalimbali. (1 Wakorintho 15:6) Ni vyepesi kupinga ushuhuda wa mutu mumoja ao wawili, lakini si vyepesi kupinga ushuhuda wa mashahidi 500 ao zaidi.

Ona pia kuwa Paulo alitaja mara mbili kwamba kufa, kuzikwa, na kufufuliwa kwa Yesu kulikuwa “kulingana na Maandiko.” Matukio hayo yote yalihakikisha kwamba unabii mbalimbali katika Maandiko ya Kiebrania juu ya Masiya ulitimia, na hilo lilionyesha kwamba Yesu alikuwa kwa kweli yule Masiya aliyeahidiwa.

Ijapokuwa ushuhuda wa watu waliomuona Yesu kisha kufufuliwa kwake na ushuhuda wa Maandiko, bado kulikuwa watu waliokuwa na mashaka juu ya ufufuo wa Yesu, na hata leo kuna wale walio na mashaka hayo. Watu fulani wanasema kwamba mwili wa Yesu uliibwa na wanafunzi wake ambao baadaye walishuhudia eti alifufuliwa. Lakini, wanafunzi hawakuwa na uwezo wala nguvu za kuwashinda wale askari Waroma ambao walilinda mwingilio wa kaburi la Yesu. Watu wengine wanasema kama masimulizi ya kwamba Yesu aliwatokea watu mbalimbali kisha kufufuliwa kwake ni hadisi tu za kutunga. Masimulizi ya kwamba Yesu alifufuliwa si hadisi za kutunga kwa sababu aliwatokea watu wengi kwa wakati tofauti-tofauti. Pia, je, ni jambo la akili kuamini kwamba mutu wa kuwazia tu angechoma samaki na kisha kuwapa watu wakule, kama Yesu alivyofanya huko Galilaya kisha kufufuliwa kwake? (Yohana 21:9-14) Je, mutu wa kuwazia tu aliyekuwa katika umbo la mwanadamu angewaomba watazamaji wake wamuguse?​—Luka 24:36-39.

Hata hivyo, wengine wanasema kwamba ufufuo wa Yesu ni uongo ambao wanafunzi wake walitunga tu. Lakini wangepata faida gani kwa kufanya hivyo? Kutoa ushuhuda juu ya ufufuo kuliwafanya wanafunzi wazarauliwe, wateseke, na hata wauawe. Sababu gani wangehatarisha maisha yao hivyo ili kuunga mukono uongo kama huo? Zaidi ya hilo, walitoa kwanza ushuhuda wao huko Yerusalemu, mbele ya wapinzani wao ambao walikuwa tayari kutafuta kisingizio chochote ili kuwahukumu.

Ufufuo lilikuwa tukio ambalo liliwapa wanafunzi uhodari wa kutoa ushuhuda juu ya Bwana wao ijapokuwa wangeteswa vikali zaidi. Uhakika wa kwamba Yesu alifufuliwa ulikuwa ndio musingi wa imani ya Kikristo. Wakristo wa kwanza hawakuhatarisha maisha yao ili tu kutoa ushuhuda juu ya mwalimu mwenye hekima ambaye aliuawa. Walihatarisha maisha yao ili kutangaza kwamba Yesu alifufuliwa kwa sababu ufufuo huo ulionyesha kama alikuwa ndiye Kristo, Mwana wa Mungu, mutu mwenye nguvu na aliye hai ambaye aliwasaidia na kuwaongoza. Ufufuo wake ulimaanisha kwamba wao pia wangefufuliwa kutoka kwa wafu. Kwa kweli, ikiwa Yesu hakufufuliwa, hakungekuwa Ukristo. Ikiwa Yesu hakufufuliwa, labda hatungesikia hata kidogo habari juu yake.

Basi, ufufuo wa Kristo una maana gani kwetu leo?

^ Katika Biblia, neno la Kigiriki linalotafsiriwa “ufufuo” linamaanisha moja kwa moja “kusimama tena.” Neno hilo linatoa wazo la kwamba mutu anarudishwa tena kwenye uzima, akiwa mutu uleule, aliye na sifa zilezile na anayekumbuka mambo yaleyale aliyofanya mbele ya kufa.

^ “Wale kumi na wawili” ni namna nyingine ya kusema “mitume,” hata ikiwa wakati fulani kisha kifo cha Yuda Iskariote, walikuwa 11 tu. Yesu alipowatokea wakati fulani, kulikuwa tu mitume 10 waliowakilisha wale 12, kwa sababu Tomasi hakuwa hapo.​—Yohana 20:24.